Rais Samia apongeza mpango wa kutokomeza magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele


Na Mwandishi Wetu
RAIS Samia Suluhu Hassan ameupongeza Mpango wa Kutokomeza Magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele (NTDs), kwa namna walivyofanikiwa kupunguza magonjwa hayo kwa kiwango kikubwa.

Pongezi hizo zilitolewa leo Jumapili, Januari 30,2022 na Naibu Waziri wa Afya, Dk. Godwin Mollel, aliyemwakilisha Waziri wa Wizara hiyo, Ummy Mwalimu kwenye kilele cha maadhimisho ya magonjwa hayo yaliyofanyika kwenye viwanja vya Nyerere Square jijini Dodoma.

“Mh Rais anatambua kazi yenu na anawapongeza sana mmefanyakazi kubwa sana kwasababu mlianza kuyapunguza kwenye wilaya 119 na sasa zimebaki wilaya tisa haya ni mafanikio makubwa sana na mnahitaji pongezi na serikali itakaa nanyinyi tuone namna ya kwenda kasi zaidi,” amesema.

Aidha amesema iwapo mpango utaweka kambi maalum kwenye Wilaya na Mikoa upo uwezekano wa kuwafanyia upasuaji wagonjwa wengi wenye mabusha na kufanikiwa kuwamaliza kabisa ifikapo mwaka 2030.

Dk. Mollel amesema kwa kuwa kwa sasa kuna wagonjwa 29,500 wenye mabusha kasi inayoendelea ya sasa haiwezi kuamaliza kwa muda mfupi hivyo alipendekeza iwekwe mikakati madhubuti kuhakikisha angalau wanawafanyia upasuaji wagonjwa 60 kwa siku.

"Kufanya upasuaji wa mabusha hakuhitaji utaalamu mkubwa sana hivyo tukijipanga tunaweza ndiyo sababu nataka mje ofisini tuweke mikakati ili tuweze kuwamaliza kwasababu idadi iliyopo ni kubwa tukienda na kasi iliyopo tutakaa sana,” amesema Naibu Waziri

Amesema kwa kuwa si kila mtanzania anaweza kumudu gharama za upasuaji wa mabusha hivyo alisema atamwomba Rais Samia Suluhu Hassan ili serikali igharamie matibabu na upasuaji kwa watu wenye ugonjwa huo.

“Haya ni mawazo yangu sijasema itakuwa hivyo lakini inabidi tukae tuone kama mawazo haya yanatekelezeka na kama tukiona inawezekana kufanyiwa upasuaji bure tutawatangazia. Najua ugumu wa kazi hii ila nataka twende kwa kasi zaidi ili watu wengi wapate huduma, yaani kama mnakimbia spidi kilomita 120 kwa saa mimi nataka twende kilomita 60 kwa saa,” amesema

Meneja Mpango huo, Dk. George Kabona amesema kwa sasa gharama ya upasuaji wa mabusha kwa mtu mmoja inakadiriwa kufikia Sh 250,000 na mpaka kufikia mwaka 2021 mpango huo umeshawafanyia upasuaji watu 8,191 na nchi nzima inakadiriwa kuwa na wagonjwa 29,500 wenye mabusha.

Amesema mwaka 2008, mpango huo ulifanikiwa kuwafanyia upasuaji wagonjwa 200, mwaka 2013 wagonjwa 680, mwaka 2015 wagonjwa 315, mwaka 2016 wagonjwa 709 na mwaka 2017 wagonjwa 1,239 wakati mwaka 2018 walifanyiwa wagonjwa 1,441.

Dk. Kabona alisema mwaka 2019 mpango huo ulifanikiwa kuwafanyia upasuaji watu 1,387, mwaka 2020 watu 1,054 wakati mwaka 2021 walifanya upasuaji kwa watu 1,116 na kwamba mpango huo ulizinduliwa mwaka 2009 kwa ushirikiano na Shirika la Kudhibiti Usubi Afrika na Shirika la Misaada la Marekani USAID.



from MPEKUZI

Comments