Rais Samia Suluhu Hassan atoa msamaha kwa wafungwa 5,704


Rais Samia Suluhu Hassan ametoa msamaha kwa wafungwa 5,704 wakiwemo walioingia gerezani wakiwa wajawazito na wenye watoto wanaonyonya, ikiwa ni kuadhimisha miaka 60 ya Uhuru wa Tanzania Bara Desemba 9, mwaka huu.

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, George Simbachawene alisema hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana.

Alisema Rais Samia ametoa msamaha huo kwa kutumia mamlaka aliyopewa kupitia Ibara ya 45 (1) d ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Alisema msamaha huo unakwenda sambamba na masharti kadhaa yakiwamo kupunguziwa robo ya adhabu zao baada ya punguzo la kawaida la theluthi moja linalotolewa chini ya kifungu cha sheria ya 49 (1) ya Sheria ya Magereza sura ya 58.

Alisema wafungwa hao sharti wawe wametumikia robo ya adhabu zao gerezani na wawe wameingia gerezani kabla ya Oktoba 9, 2021.

Wengine wanaohusika katika msamaha huo ni wafungwa wenye magonjwa ya kudumu ambao hawana uwezo wa kufanya kazi na ugonjwa uwe umethibitishwa na jopo la waganga wa mkoa na wilaya.

Simbachawene alisema wafungwa wengine watakaofaidika na msamaha huo ni wazee wenye miaka kuanzia 70 na kuendelea na umri huo uwe umethibitishwa na jopo la waganga wakiongozwa na mwenyekiti wa waganga wa mkoa na wilaya.

“Wafungwa wote wa kike walioingia na mimba pamoja na wale walioingia na watoto wanaonyonya na wasionyonya. Wafungwa wenye ulemavu wa mwili na akili na ulemavu huo uwe umethibitishwa na jopo la waganga wa wilaya na mkoa nao wanahusika,” alisema.

Alisema wengine watakaofaidika na msamaha huo ni waliokaa miaka 20 na kuendelea gerezani na ambao wameonesha tabia njema pamoja na waliowahi kunufaika na msamaha wa Rais pamoja na waliohukumiwa kukaa kizuizini na wamekaa kwa miaka 15 na kuendelea watahusika pia katika msamaha huo.

Kwa mujibu wa Simbachawene, msamaha huo hautahusisha wafungwa wakiwemo waliohukumiwa kunyongwa, wenye makosa

ya kujaribu kujiua, kuua au kuua watoto wachanga, wanaotumikia vifungo chini ya bodi ya parole na waliopatikana na hatia na kuhukumiwa kwa kutumia sheria ya uhujumu uchumi.

Alisema wafungwa wengine ambao hawatanufaika na msamaha huo ni pamoja na vifungo vya matumizi mabaya ya madaraka na utakatishaji wa fedha, rushwa na usafirishaji wa binadamu, utekaji na wizi wa watoto.

Wafungwa waliohukumiwa kwa kuwapa mimba wanafunzi pamoja na waliopatikana na hatia na kufungwa kwa kosa la unyanyasaji wa

watoto, kukutwa na viungo vya binadamu, wafungwa wanaotumikia makosa ya kupatikana na nyara za serikali na wizi na ubadhirifu wa mali za umma pia hawatanufaika na msamaha huo.

Msamaha huo pia hautawahusu wafungwa waliofungwa kwa kujaribu kutoroka chini ya ulinzi halali pamoja na wafungwa waliopata msamaha wa Rais na hawakufikisha miaka 10 tangu wapate msamaha huo.




from MPEKUZI

Comments