Fanyeni Kazi Kwa Kuzingatia Weledi : Jaji Kiongozi

Na Innocent Kansha Kilindi Mahakama
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt Eliezer Mbuki Feleshi amewataka Watumishi wa Mahakama ya Tanzania kufanya kazi kwa kujituma, kujitolea, na kushirikiana.

Akizungumza na watumishi wa Mahakama ya wilaya ya Kilindi jana wakati wa ziara yake ya kikazi wilayani humo, Jaji Kiongozi pia amewataka watumishi hao kuzingatia maadili wanapotekeleza majukumu yao ili kujenga taswira chanya ya Mahakama kwa wananchi.

“Ombeni kupewa kazi za ziada kwa viongozi wenu pale mnapoona kituo husika hakina mashauri mengi, hata kumsaidia Hakimu Mfawidhi kufanya utafiti ili kurahisisha kutoa maamuzi kwa wakati au vituo vya jirani ili kuboresha utendaji”, alisema Jaji kiongozi.

Jaji Feleshi aliwashauri watumishi kuanzisha vikao vya kitaaluma ili kujengeana uwezo katika fani zao. Alisema Sheria na kanuni zimekuwa zikifanyiwa marekebisho mara kwa mara hasa kwa miaka ya hivi karibuni ikiwemo sheria ya mwenendo wa madai na sheria za Mahakama za mahakimu ili kutafuta na kupata ubobezi kwenye taaluma.

“Hakuna Hakimu wa mjini wala wa kijijini wote nyinyi ni wamoja kwenye suala la kutafsiri sheria zilizotungwa na Bunge na kanuni zake, vikao hivi vitawasaidia kuwajengea uwezo na uelewa wa kuendesha shughuli zenu za kila siku za utoaji haki kwa wananchi”, alisistiza Jaji Kiongozi.

Mhe. Jaji Feleshi aliwahimiza watumishi kuzingatia maadili, kufanya kazi kwa bidii, na kuonyesha uadilifu kwa vitendo waendelee kutenda haki. Aliwataka viongozi kusimamia kikamilifu na kutumia busara katika kulea, kuonya, kutoa ushauri na kueleza ukweli.

Aidha, Jaji Feleshi pia amewataka viongozi kusimamia masuala yote yanayowahusu watumishi na kuyapa kipaumbele ikiwa ni pamoja na kujenga mahusiano mazuri mahala pa kazi, kuzifahamu changamoto zao na kuzitafutia ufumbuzi kwa wakati. Aliongeza kuwa endapo viongozi watakuwa wakiwaelimisha watumishi haki zao za msingi watasaidia kuondoa malalamiko yasiyo ya msingi.

Mhe. Dkt Feleshi aliwataka watumishi kuendelea kuwahudumia wateja bila kuchoka na kuacha kutumia lugha zisizofaa.” Wadau wetu wengi mara nyingi wanapofika mahakamani huwa na mitazamo tofauti hivyo wakieleweshwa wataelewa na kuondoa migongano na manung’uniko yasiyo ya lazima”, alisema.

Wakati huo huo Jaji Kiongozi alikutana na Mkuu wa Wilaya ya Kilindi Bi. Sauda Mtondoo Ofisini kwake na viongozi wa kamati ya Ulinzi na Usalama ya wilaya na kufanya mazungumzo ambapo Mkuu huyo wa wilaya aliishukuru Mahakama ya Tanzania kwa kuanzisha Mahakama ya Wilaya ya Kilindi baada ya maombi ya muda mrefu.

Akizungumza na Mkuu huyo wa wilaya, Jaji Kiongozi alisema Mahakama kwa sasa imejiimarisha na inasisitiza matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika kurahisisha shughuli zake za kila siku za utoaji haki.

“Mfumo huu umesaidia kurahisisha uendeshaji wa mashauri na kupunguza gharama kwa kiasi kikubwa kwa upande wa wadau na Mahakama, hivyo tembeleeni mifumo ya Mahakama ili kujua mambo mengi yanayofanyika”, alisema.

Jaji Kiongozi pia alitembelea eneo linalojengwa Mahakama ya Wilaya ya Kilindi na kupokea taarifa ya maendeleo ya ujenzi wa jengo la Mahakama hiyo kutoka kwa Mtendaji wa Mahakama ya Tanzania Kanda ya Tanga.

Jaji Kiongozi ameanza ziara ya siku tano Mahakama Kuu ya Tanzania kanda ya Tanga ambapo atakagua shughuli mbalimbali zinazofanywa na Mahakama.


from MPEKUZI

Comments