Waasi wa Syria wanaoungwa mkono na Uturuki wadhibiti mji ulio karibu na Idlib

Waasi wa Syria wanaoungwa mkono na jeshi la Uturuki wamedhibiti mji wa Narab, katika mkoa wa Idlib, kwa mujibu wa vyanzo kutoka Uturuki na wawakilishi wa waasi.

Vikosi vya rais Bashar al-Assad, ambavyo vinaungwa mkono na jeshi la anga la Urusi, wanajaribu kuiteka ngome hii ya mwisho ya waasi nchini Syria baada ya miaka tisa ya vita.

Karibu raia milioni moja wameyahama makazi yao tangu kuanza tena kwa mashambulizi ya vikosi vya serikali vya Syria na mshirika wake Urusi Desemba mwaka jana, kulingana na takwimu za Umoja wa Mataifa.

Vikosi vya serikali vimeuteka mji wa Kafr Nabel na maeneo jirani, yanayopatikana karibu kilomita 30 Kusini Magharibi mwa Nairab, shirika la Haki za Binadamu nchini Syria (OSDH), chanzo cha eneo hilo na vyombo vya habari vimeripoti.

Uturuki imetuma maelfu ya askari na vifaa katika mkoa huo kusaidia waasi wa Syria, na kuongeza mvutano na Urusi, mshirika mkuu wa Syria.


from MPEKUZI

Comments