Mwanafunzi Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) Ahukumiwa Jela Miezi 12 au Faini Milioni 5 Kwa Kuchapisha Maudhui Mtandaoni Bila Leseni

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam nchini Tanzania, imemhukumu mwanafunzi wa mwaka wa pili, Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) Julius Warioba (23) kulipa faini ya Sh5 milioni au kwenda jela mwaka mmoja.

Ni baada ya kukiri shtaka la kuchapisha maudhui katika Mtandao bila kuwa na leseni kutoka Mamlaka ya Udhibiti wa Mawasiliano Tanzania (TCRA).

Warioba ambaye ni mshereheshaji (MC) anadaiwa kuchapisha maudhui kupitia Televisheni ya mtandaoni  inayojulikana kwa jina Mc Warioba, bila kuwa na kibali kutoka TCRA wakati wakijua kuwa ni kinyume cha sheria ya Mtandao.

Mbali na faini, Mahakama hiyo, imetaifisha kompyuta aina ya Apple na simu ya mkononi aina ya Iphone ambavyo vilitumika katika kuchapisha maudhui hayo.

Hata hivyo, mshtakiwa huyo amefanikiwa kulipa faini na hivyo kukwepa kifungo.

Hukumu hiyo imetolewa jana  Jumatatu Agosti 26, 2019 Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama hiyo, Janeth Mtega baada ya mshtakiwa kutiwa hatiani.


from MPEKUZI

Comments