Wasiooga na Kufungua Nguo Wapigwa Marufuku Jijini Dar

Mkuu  wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, amepiga marufuku watu wasiooga na kuwa nadhifu kuingia katikati ya jiji hilo wakati wa mkutano wa 39 wa nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) mwezi ujao.

Tayari vijana 130 wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) na mgambo 300 wamesambazwa maeneo mbalimbali ya jiji hilo kusimamia usafi wa mazingira.

Akizungumza jana wakati wa kuzindua kampeni ya usafi wa mazingira kama sehemu ya maandalizi ya mkutano huo, Makonda alisema wamejipanga vyema, hasa katika suala zima la usafi kuepuka kumtia aibu Rais Dk. John Magufuli mbele ya marais wenzake.

“Wakati wa mkutano huu hatutarajii kuona watu wachafu mtaani. Tabia ya kuja mjini hujafua, hujaoga, hujanyoosha nguo ni marufuku, mpumzike tu majumbani kwenu.

“Kwa kipindi hiki tuvumiliane, kama hufui nguo, huogi, pumzika kidogo kuja mjini usitutie aibu, na siyo kwamba tunataka usafi tu wa mazingira hapana, usafi pia wa wananchi wetu, watu wamejaa chawa tu hapa,” alisema Makonda.

Pia aliagiza kuanzia sasa wenye magari binafsi watakaotupa taka ovyo wasitozwe faini badala yake wapewe eneo la kufanya usafi kwani baadhi yao wamekuwa na jeuri ya fedha na kwamba kwao faini si adhabu.


from MPEKUZI

Comments