Serikali yapiga marufuku walimu wa Madarasa ya Awali kuingia na viboko darasani

NA TIGANYA VINCENT
SERIKALI imetoa wito kwa wadau wa elimu kushirikiana na Serikali katika kujenga mazingira mazuri ya utoaji wa elimu nchini ikiwemo ujenzi wa madarasa, vyoo na nyumba za walimu.

Kauli hiyo imetolewa jana mjini Mwanza na Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) - anayeshughulikia Elimu Tixon Nzunda wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha kuandaa vipindi vya redio kupitia Mpango wa Kuinua Ubora wa Elimu Tanzania (MKUE-Tanzania)

Alisema hali ilivyo sasa ili kukamilisha miundombinu na kuweka mazingira mazuri ya utaoji wa elimu na ujenzi wa nyumba za kuishi walimu zinahitajika shilingi trilioni 14 kutekeleza zoezi hilo katika Shule za Sekondari na Msingi nchini kote.

Nzunda alisema Serikali pekee yake haiwezi kukamilisha zoezi hilo bila kushirikiana na wadau wengine ili kujenga madarasa ya kutosha ili kupunguza msongamano wa wanafunzi, kuondioa uhaba wa nyumba za walimu na vyoo.

Alisema Serikali katika kukabiliana na tatizo la msongamano wa wanafunzi katika shule mbalimbali za Msingi na Sekondari tayari katika kipindi cha miezi mitatu iliyopita imetoa zaidi ya bilioni 65 kwa ajili ya ujenzi wa maboma ya madarasa 5,289  nchini kote.

Nzunda alisema kuwa  fedha hizo zimesaidia kukamilisha maboma 2,392 kwa ajili ya Sekondari  na 2,897 ni kwa ajili ya Msingi nchini kote.

Katika hatua nyingine Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) -  anayeshughulikia Elimu amepiga marufuku kwa walimu wanaofundisha  madarasa ya kuanzia elimu ya awali hadi darasa la tatu kuingia na viboko madarasa.

Alisema kuwa vitendo hivyo vinasababisha wanafunzi wa madarasa hayo kuogopa na kutokuwa wasikivu wakati wa wanapofundishwa.

Kuhusu Mpango wa Kuinua Ubora wa Elimu Tanzania (MKUE-Tanzania) alisema kuwa umechangia katika kuboresha elimu katika mikoa 9 kiwango cha ufaulu kwa shule za Msingi umeongezeka kutoka chini asilimia  40 hadi kuwa  juu ya 77 na maeneo mengine kufikia asilimia  100.

Mafunzo hayo ya siku tatu kupitia Mpango wa Kuinua Ubora wa Elimu Tanzania (MKUE-Tanzania) yanayowashirikisha waandishi wa habari, Maafisa Elimu Mikoa na Maafisa Habari kutoka Mikoa 9 yameandaliwa na TAMISEMI kwa kushirikiana na Wizara ya Maendeleo ya Kimataifa ya Uingereza(DFID)

 


from MPEKUZI

Comments