MOI Mwenyeji Kongamano la Kimataifa la Madaktari Bingwa wa Mifupa zaidi 150

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Tiba ya Mifupa MOI Dkt Respicious Boniface  jana amefungua kongamano la kimataifa la madaktari wa Mifupa linalofanyika kwa siku tano hapa Tanzania ambapo madaktari zaidi ya 150 kutoka mataifa ya Afrika na sehemu mbalimbali duniani wanashiriki.
 
Dkt Boniface amesema Kongamano hilo limekua likifanyika hapa nchini kila mwaka kwa lengo la kuwajengea uwezo na kuwapa mbinu mpya za matibabu ya mifupa madaktari hapa nchini na nchi nyingine barani Afrika kutokana na MOI kuwa kituo cha mafunzo kutokana na huduma bora za mifupa inazotozitoa.
 
“Madaktari bingwa wetu hapa nchini wamekua wakinufaika sana na kongamano hili, wamekua wakipewa mbinu mpya na zakisasa za matibabu na upasuaji wa mifupa jambo ambalo limepelekea MOI kuweza kumaliza rufaa za nje ya nchi kwa wagonjwa wa mifupa ambapo kwa sasa huduma karibia zote zinapatikana hapa nchini” Alisema Dkt Boniface.
 
Mratibu wa Kongamano hilo Dkt Joseph Mwanga amesema mafunzo yatatolewa kwa njia ya nadharia, vitendo katika chumba cha maabara kwa kutumia mifupa bandia na kwenda kwenye chumba maalum cha kujifunzia kwa kutumia miili ya binadamu (Cadavers).
 
“Kongamano hili limekua na manufaa makubwa sana kwetu, tumekuwa tukipata mbinu mpya kila mwaka kutoka kwa wenzetu wa Marekani jambo ambalo limefanya huduma za mifupa hapa nchini ziendelee kuwa bora ukilinganisha na mataifa mengine barani Afrika” Alisema Dkt Mwanga.
 
Kwa upande wake Profesa Michael Terry ambaye ni mkufunzi kutoka Chuo Kikuu cha Calfonia cha San Francisco amesema ushirikiano kati ya Taasisi yake na MOI umejikita katika mafunzo ya namna ya kuwahudumia majeruhi wa ajali kwa lengo la kuwapa huduma bora na za kisasa kwa wakati.
Kongamano hilo limeratibiwa na Taasisi ya MOI kwa kushirikiana na Taasisi za IGOT, SIGN, OTA, AO Alliance na Chuo kikuu cha Calfonia San Fransisco Marekani.
 
Imetolewa na
Kitengo cha Uhusiano MOI


from MPEKUZI

Comments