Mifuko Ya Fidia Kwa Wafanyakazi Ya Zambia Na Tanzania Yasaini Mkataba Wa Ushirikiano

NA Mwandishi wetu, Dodoma
TANZANIA na Zambia kupitia Mifuko ya Fidia kwa Wafanyakazi, wamesaini mkataba wa ushirikiano utakaosaidia kubadilishana uzoefu kati ya mifuko hiyo.

Akizungumza mara baada ya kutiliana saini mkataba huo, kwenye ofisi za WCF jijini Dodoma Jumatatu Mei 27, 2019, Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Bw. Masha Mshomba alisema, Zambia inauzoefu wa zaidi ya miaka 40 katika sekta ya hifadhi ya jamii katika kulipa mafao ya Fidia kwa Wfanyakazi kwa hivyo makubaliano hayo yana manufaa makubwa.

Alisema makubaliano hayo ni ya kawaida kati ya mifuko na kwamba WCF na WCFCB watabadilishana uzoefu katika masuala ya namna ya ulipaji mafao, namna ya kuzuia ajali na magonjwa kazini kwa sababu mambo hayo ni muhimu sana katika mifuko ya fidia.

“Nguvu kazi ya taifa inapolindwa tija huongezeka makazini na jambo hili hudhihirika pale pato la taifa linaongezeka hususan kwetu sisi ambao tunajenga uchumi wa viwanda jambo hilo ni muhimu sana.”Alisema Bw. Mshomba.

Alisema kwa uzoefu ambao Zambia watakuwa wameupata kutoka kwao wataweza kuboresha huduma zao, na tayari Dkt. Nkumbula amethibitisha kuwa serikali ya Zambia inautegemea Mfuko huo katika kusaidia nguvu kazi ya taifa.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi Zambia (WCFCB), Dkt. Elizabeth Lungu Nkumbula alisema, imekuwa ni siku njema kwao kwa kujenga ushirikiano wa pamoja katika eneo la hifadhi ya jamii.

“Zambai na Tanzania chini ya uongozi wa Dkt. Keneth Kaunda na Mwalimu Nyerere, waliweza kujenga reli ya TAZARA na bomba la mafuta TAZAMA kwa hivyo ushirikiano huu wa leo ni kumbukumbu ya ushirikiano uliojengwa kwa muda mrefu na viongozi hao wa mataifa hayo mawili.” Alifafanua.

AlIsema ushirikiano huu utasaidia pande mbili kubadilishana uzoefu katika kutoa huduma za ulipaji fidia na mbinu za kuzuia majanga yatokanayo na kazi na hivyo kusaidia mataifa hayo kukuza uchumi.


from MPEKUZI

Comments