Dereva Teksi Afikishwa Mahakamani kwa Tuhuma za Kumteka Mo Dewji

Dereva teksi, Mousa Twaleb (46) amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu leo Jumanne Mei 28, 2019 akikabiliwa  na mashtaka matatu likiwemo la  kumteka mfanyabiashara, Mohamed Dewji ‘Mo’.

Akisomewa mashtaka na Wakili wa Serikali Mkuu, Paul Kadushi kwa kushirikiana na Wakili wa Serikali Simon Wankyo, mshtakiwa anadaiwa kutenda makosa hayo kati ya Mei Mosi mwaka 2018 na Oktoba mwaka huo jijini Dar es Salaam na Johannesburg, nchini Afrika Kusini.

Kadushi amedai mshtakiwa alijihusisha na genge la uhalifu, walimteka Mo katika Hoteli ya Colleseum iliyopo wilayani Kinondoni na kumficha.

Mshtakiwa huyo pia anadaiwa kutakatisha Sh milioni nane ambazo alijipatia huku akijua zinatokana na mazalia ya kosa la uhalifu.

Mshtakiwa huyo hakutakiwa kujibu lolote sababu mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo. Kesi imeahirishwa hadi Juni 11, mwaka huu kwa ajili ya kutajwa.


from MPEKUZI

Comments