Serikali Yasitisha Uhamisho wa Walimu

Serikali imezuia uhamisho wa walimu nchi nzima ikieleza kuwa sababu za kuomba hivyo nyingi ni za uongo.

Naibu Waziri Ofisi ya Rais Tamisemi,  Mwita Waitara amesema hayo bungeni jana  Alhamisi Aprili 25,  akieleza kuwa kuanzia sasa uhamisho utatolewa kwa kibali maalumu na masharti muhimu kutoka serikalini.

Alikuwa akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Mrimba (Chadema), Suzan Kiwanga ambaye amehoji kuhusu upungufu wa walimu hasa wa kike katika wilaya ya Kilombero.

"Suala la kuhamisha walimu kwa uhamisho wa ndani liko chini ya mkurugenzi na hapa ninaagiza kufanyika marekebisho hayo mara moja tena ndani ya miezi miwili au wiki mbili ili kupata walimu kwa jinsia zote," amesema.

Waitara amesema Serikali imefikia hatua ya kuzuia uhamisho kutokana walimu wengi kusingizia kuwa wanawafuata wenza wao na kugundulika kuwa sababu nyingi ni za uongo.

Katika swali la msingi, Mbunge Viti Maalum (CCM), Ferister Bura alitaka kujua ni lini Serikali itaajiri walimu 527 wa masomo ya sayansi katika mkoa wa Dodoma.

Akijibu, Waitara alisema ni kweli Dodoma ina upungufu wa walimu lakini Serikali imeshatoa kibali cha kuajiri walimu 4,549 wakiwamo walimu wa sayansi na hisabati.


from MPEKUZI

Comments