Serikali Kuendelea Kuyafutia Usajili Maduka ya Kubadilishia Fedha Yasiyokidhi Vigezo

Serikali imesema ni maduka 109 nchini ya kubadilisha fedha ndiyo yaliyokidhi vigezo vya sheria mpya kwa biashara hiyo.

Waziri wa Fedha na Mipango, DK Philip Mpango ametoa kauli hiyo leo Jumapili Jijini Dodoma wakati akitoa taarifa ya hali ya uchumi wa taifa na utekelezaji wa bajeti ya Serikali katika nusu ya kwanza ya mwaka wa fedha 2018/19.

DK Mpango amesema kabla ya kufanya usajili mpya, kulikuwa na jumla ya maduka ya kubadilisha fedha 297 nchi nzima.

Amesema jumla ya maduka 188 yalishindwa kutimiza masharti na hivyo kupelekea kufutiwa usajili wao huku akiahidi kuendeleza msako zaidi kwenye maduka yote nchini.

"Serikali kupitia (Benki Kuu ya Tanzania) BOT imeendelea kuchukua hatua za kuimarisha biashara ya kubadilisha fedha za kigeni ili kuondoa uwezekano wa maduka makubwa haya kufanya biashara isiyo halali ambayo ni pamoja na utakatishaji wa fedha haramu," amesema Mpango

Ametaja baadhi masharti yaliyowaondolea leseni ni kuwekwa kwa sharti la kiwango cha chini kwa maduka yaliyo katika daraja A kuwa ni mtaji wake uwe Sh100 milioni hadi Sh300 milioni wakati daraja B iwe Sh250 milioni hadi Sh1 bilioni.


from MPEKUZI

Comments