Mawaziri wakutana Mbeya kumpongeza Rais Magufuli

Mawaziri wameungana kumpongeza Rais John Magufuli kwa utekelezaji wa miradi mbalimbali nchini kwa kasi kubwa.

Pongezi hizo zimetolewa leo Jumamosi Desemba 29, 2018 jijini Mbeya katika kongamano la Jumuiya ya Umoja wa Wanawake wa Chama cha Mapinduzi (UWT) lililofanyika kitaifa jijini humo.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako amesema Rais Magufuli amefanya kazi kubwa kuhakikisha elimu inapatikana kwa wote bila kujali hali zao kiuchumi.

"Mheshimiwa Rais ameweza kusaidia kutolewa kwa elimu bure jambo lililopelekea ongezeko la watoto wanaoandikishwa katika shule zetu," amesema Profesa Ndalichako.

Naye Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Angellina Mabula amesema Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Magufuli imesaidia kwa kiasi kikubwa kutatua migogoro mbalimbali ya ardhi.

"Serikali inaandaa mfumo ambao utasaidia kuondokana na tatizo la ardhi kumilikiwa na mtu zaidi ya mmoja," amesema Mabula.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Maji, Juma Aweso amesema miradi iliyotakiwa kutekelezwa katika awamu hii ni 1,810 lakini mpaka sasa miradi 1,659 imekwisha kutekelezwa.


from MPEKUZI

Comments