Jeshi la Polisi Dar Latoa Dakika Tano za Kuoiga Fataki Mwaka....Latoa Onyo Utapeli Unaoendelea Nchini

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dar es salaam Lazaro Mambosasa amebainisha kuwa katika kipindi cha mwaka mmoja Jeshi hilo limefanikiwa kukusanya zaidi ya shilingi bilioni 29, zilizotokana na makosa mbalimbali ya usalama barabarani ambayo watuhumiwa wake walikiri kufanya.

Mambosasa ameyasema hayo leo Desemba 31, 2018, Jijini Dar es salaam wakati akitoa taarifa ya utekelezaji wa jeshi hilo na mafanikio yake katika kipindi cha mwaka mmoja.

"Kipindi cha mwaka mmoja fedha tulizofanikiwa kukusanya ni bilioni 29, kwa watuhumiwa wa makosa ya kukamatwa kwa vyombo vya usafiri na wenyewe wakakiri kufanya makosa hayo".

Aidha Kamanda Mambosasa ameogeza, "naomba wadau tushirikiane kwa pamoja kuhusu wahamiaji haramu, kwa hapa DSM kuna wimbi kubwa la matapeli ambao ni raia wa kigeni na wanafanya uhalifu, hili eneo si la kufumbiwa macho, unakuta mstaafu katoka kuchukua kiinua mgongo, anatapeliwa".

"Wanachi wanaumizwa kweli mmoja hapo chini kuna mstaafu ametapeliwa milioni 120, na mnigeria ambaye ameingia nchini na anaishi bila kibali."

Katika hatua nyingine Kamanda Mambosasa amewaonya wananchi watakaosherehekea mkesha wa mwaka mpya kwa kufyatua mafataki badala yake ametoa dakika 5 kwa watakaotaka kufanya tukio hilo kuanzia saa 6 kamili usiku hadi saa 6.05 usiku.

“Milipuko yoyote hatutaruhusu isipokuwa kwa wale waliopewa kibali hasa kwenye mahoteli ya nyota tano. Hawa ndio watakaofyatua fataki tena ziwe nyepesi na si nzito,” amesema Mambosasa.

“Wakati wakiendelea na ufyatuaji, polisi watakuwepo eneo husika na atakayekwenda kinyume na maagizo atachukuliwa hatua.”

Mambosasa amewaonya wananchi kutochoma matairi kwenye barabara, watakaobainika watakamatwa.


from MPEKUZI

Comments