Tazama Hapa Mapingamizi Matatu Yaliyotolewa na Upande wa Jamhuri Katika Rufaa ya Freeman Mbowe na Ester Matiko

 Upande wa Jamhuri katika rufaa ya dhamana ya Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na Mbunge wa Tarime Mjini, Esther Matiko umepinga rufaa hiyo na kutoa sababu za kufanya hivyo.

Jamhuri imeweka pingamizi la awali ikiwasilisha hoja tatu za kutaka rufaa hiyo itupiliwe mbali bila hata kusikiliza msingi wake.

Katika hoja ya kwanza, Wakili wa Serikali Mkuu, Dk Zainabu Mango amesema kuwa taarifa ya kusudi la kukata rufaa si sahihi.

Amesema kifungu cha sheria kilichotumika katika taarifa ya kusudio la kukata rufaa hakiipi Mahakama mamlaka ya kusikiliza rufaa hiyo kwa sababu siyo sahihi, hivyo inapaswa kutupiliwa mbali.

Katiika hoja ya pili, Wakili wa Serikali, Wankyo Simon amesema rufaa hiyo haijakidhi matakwa ya kisheria kifungu cha 362 (1) kuhusu mwenendo wa shauri kuambatanishwa katika rufaa.

Amesema mwenendo wa mambo mengi yaliyotokea siku za nyuma tangu kesi ya msingi ilipofunguliwa ambazo Mahakama ingezipata zingesaidia kuiongoza vyema Mahakama kutenda haki.

Amesema masharti ya dhamana ambayo kwa mujibu wa kifungu hicho yanaweza kukatiwa rufaa lakini tangu yalipotolewa kati ya Machi na Aprili mwaka huu hayajawahi kukatiwa rufaa, kuwasilisha taarifa ya kusudio la kukata rufaa wala kuomba kuongezewa muda wa kukata rufaa.

Wakili Nchimbi amesema kwa hali hiyo inaonyesha kuwa wakata rufaa waliridhika na masharti hayo na hivyo haiwezekani kuja kuyaibua leo.

Baada ya hoja hizo, Mahakama kuu imesema  Kesho November 30, 2018  itatoa  uamuzi kama itatengua uamuzi wa Mahakama ya Kisutu ama kukubali .
 
Mbowe ambaye ni Mbunge wa Hai na Matiko wamekata rufaa Mahakama Kuu kupinga uamuzi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwafutia dhamana katika kesi ya jinai inayowakabili mahakamani hapo.


from MPEKUZI

Comments