Tazama Hapa Kilichoamuriwa Leo Mahakamani Kuhusu Rufaa ya Mbowe na Matiko

Jaji Sam Rumanyika anayesikiliza kesi ya pingamizi la rufaa ya kupinga uamuzi wa kufutiwa dhamana ya Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe na Mbunge wa Tarime Mjini, Ester Matiko, amepiga simu Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akiamuru mwenendo wa kesi na uamuzi uliowafutia dhamana washtakiwa hao umfikie ofisini kwake haraka.

Jaji Rumanyika alifanya hivyo leo Jumatano Novemba 28, baada ya rufaa kukwama kusikilizwa kwa sababu nyaraka hizo hazikuambatanishwa na jalada lililomfikia.

Alipiga simu  kwa karani wa mahakama baada ya kukosa namba ya Hakimu

Baada ya simu kupokelewa Jaji Rumanyika alijitambulisha kwa majina huku sauti ya upande wa pili (sauti ya karani Comas) ilisikika akiitikia kumfahamu.

Jaji Rumanyika alimuuliza kama anaifahamu kesi Namba 112/2018 naye akajibu anaifahamu, kisha akauliza kwanini nyaraka zilizomfikia hazijakamilika, hakuna uamuzi wa mahakama na mwenendo wa kesi.

Karani alijibu kwamba bado hazijamaliziwa kuchapwa na Jaji Rumanyika alitaka ampelekee hivyo hivyo ziwe zimechapwa au zimeandikwa kwa mkono.

“Nenda unileee nakusubiri ofisini kwangu chumba namba 16… Nasubiri, “Jaji Rumanyika ilikata simu na kuzitaka pande zote mbili kusubiri hadi saa saba wajiridhishe kupata nyaraka hizo.

Rufaa hiyo itaanza kusikilizwa kesho Alhamisi asubuhi. Washtakiwa walirudishwa rumande.


from MPEKUZI

Comments