Mazingira Bora Ya Miradi Kuipatia Mikopo Sekta Binafsi Tokaka Katika Mashirika Ya Kimataifa

Na. WFM, Bali Indonesia
Mazingira bora yakutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo katika Sekta Binafsi kutaiwezesha sekta hiyo kupata fedha katika Mashirika ya Kimataifa ambayo yametenga bajeti kwa ajili ya kuimarisha sekta hiyo.

Hayo yameelezwa mjini Bali Indonesia na Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Isdor Mpango, baada ya kumalizika kwa  mikutano ya mwaka ya Benki ya Dunia (WB) na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) iliyowakutanisha Mawaziri wa Fedha na Magavana wa Benki Kuu wa nchi mbalimbali.

Dkt. Mpango alisema kuwa, yapo Mashirika ambayo yapotayari kutoa fedha iwapo kuna uhakika wakurudishwa kwa fedha hizo kama zitatolewa kwa mfumo wa  mikopo, hivyo ni vizuri mazingira ya utekelezaji miradi ya Sekta Binafsi yakaboreshwa ili kuwe na urahisi wa upatikanaji wa fedha hizo.

Alisema kuwa, nchi za Afrika ikiwemo Tanzania zinahitaji pia fedha za kuwekeza kwenye miundombinu ya kiteknolojia ili kuweza kuchochea ukuaji wa uchumi

“Kama nchi inatakiwa kuhakikisha  inaongeza mapato ya ndani ya kodi  na yasiyo ya kodi kwa kuwa jambo hilo ni moja ya kigezo chakuweza kupata fedha zaidi kutoka Mashirika ya Kimataifa”, alieleza Dkt. Mpango.

Naye Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Dkt. Yamungu Kayandabila, alisema kuwa katika mikutano ya mwaka ya WB na IMF, imesisitiza kuondoa vikwazo vya kibiashara kati ya nchi na nchi  kwa kuwa biashara imekuwa na mchango mkubwa katika kukuza pato na uchumi wa nchi unategemea mahusiano mazuri kati ya taifa moja na lingine.

Dkt. Kayandabila alisema kuwa, Mataifa makubwa ikiwemo China na Marekani yanatakiwa kupunguza mvutano unaosababishwa na vikwazo vya kodi baina yao ili kutoathiri nchi ndogo ikiwemo Tanzania inayofanya biashara na nchi hizo.

Mikutano ya Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa imemalizika mjini Bali Indonesia kwa Mkurugenzi Mtendaji wa IMF Bi. Christine Lagarde na Rais wa Benki ya Dunia Bw. Jim Yong Kim, kukutana na Mawaziri wa Fedha na Magavana wa Benki Kuu ambapo waliangazia mwenendo wa uchumi wa ulimwengu hasa Afrika ambayo uchumi wa baadhi ya nchi unaenda vizuri na nyingine kutofanya vizuri na kusababisha Bara hilo kuonekana uchumi wake kuonekana kukua kwa kasi ndogo.


from MPEKUZI

Comments