Askofu Wa Kanisa La Mungu Awaombea Wanafunzi Kidato Cha Nne

Na John Walter-Babati
Wakati wanafunzi wa kidato cha nne kote  nchini wakijiandaa kufanya mitihani yao ya mwisho ya kuhitimu mwezi oktoba mwaka huu, wazazi wametakiwa kuwa karibu na watoto wao pamoja na kufuatilia mwenendo mashuleni.

Wito huo umetolewa na Makamu Askofu Mkuu wa kanisa la Mungu la Tanzania Askofu Boniface Msufa, alipokuwa akizungumza na wazazi,walimu na wanafunzi wa kidato cha nne katika Mahafali ya 18 ya shule ya sekondari Aldersgate iliyopo mjini Babati mkoani Manyara yaliyofanyika mwishoni mwa wiki.

Askofu Msuva aliwataka wazazi kushiriki kwa pamoja kuwaombea wanafunzi wa kidato cha nne katika mitihani yao ili waweze kufanya vyema.

“Kwa sasa hivi kwa sera ya nchi yetu elimu hiyo mliyonayo ni elimu ya msingi,elimu ya awali kwa hiyo bado kuna safari mbele mnahitaji kukazana zaidi”alisema askofu Msufa.

Akizungumzia mafanikio waliyoyapata mpaka sasa mkuu wa shule hiyo Mwalimu Fredson Dillo, amesema shule imefanikiwa kuwa na mradi wa Ng’ombe wa Maziwa na nyama pamoja na kuanzisha programme ya wanafunzi kusoma kupitia mitandao inayojulikana kama E-Learning.

Akizungumzia matokeo ya kidato cha nne mwaka 2017  alisema, Division one zilikuwa 2,Division two 35,Division three 34 na Division four 6,Division 0 haikuwepo,kwa hiyo tulifaulu kwa asilimia 100% na jumla ya watahiniwa walikuwa 97.

Mwalimu Dillo ameeleza kuwa katika matokeo ya kidato cha nne  mwaka 2017 shule ilishika nafasi ya nne Kimkoa kati ya 180, 108 Kimkoa na 249 kati ya shule 3280 Kitaifa.

Shule ya Sekondari Aldesgate ambayo ipo chini ya Kanisa la Mungu La Tanzania yenye namba ya Usajili S-941 na namba ya mtihani S- 1093 ni ya mchepuo wa Biashara na Sayansi, ambayo ina walimu  wa kike 6 na wa kiume  27 ambao wanawahudumia wanafunzi 738, wavulana wakiwa 388 huku wasichana wakiwa 370 na  inaendeshwa kwa kuzingatia kanuni na sheria zote za wizara ya elimu kuanzia kidato cha kwanza hadi cha sita.

Kwa upande wa meneja msaidizi wa Bank  of Afrika tawi la Babati mjini Julius Mnkande aliwasihi wanafunzi kusoma kwa bidii ili kuendana na soko la ajira ambalo linahitaji wasomi na kuepuka vishawishi ambavyo vitawasababishia kushindwa kufikia malengo yao katika elimu.

Jumla ya wanafunzi 127 wa kidato cha nne katika shule ya Sekondari Aldersgate,wasichana 59 na wavulana 68 wanatarajia kufanya mitihani yao ya kuhitimu kidato cha nne.


from MPEKUZI

Comments