Maofisa wa Marekani Wadai Korea Kaskazini Bado Inaendelea Kuunda Makombora Mapya

Korea kaskazini inaonekana kuwa inaunda makombora mapya licha ya kuidhinisha uhusiano mwema na utawala wa Trump, vyombo vya habari vinaripoti.

Satelaiti za kijasusi zimegundua shughuli zinazoendelea katika eneo ambako kumetengezwa makombora ya masafa marefu, maafisa wa Marekani wameliambia Washington Post.

Shirika la habari la Reuters linamnukuu afisa huyo akisema kuwa haijulikani wazi ni kwa kiwango gani shughuli hiyo imeendelea.

Rais Donald Trump amekutana na kiongozi wa Korea kaskazini Kim Jong-un mnamo Juni. Baada ya mkutano wa kwanza, viongozi hao wawili waliahidi kushughulika kuhakikisha wanasitisha matumizi ya silaha za nyuklia. Trump alisema Korea kaskazini, 'sio tishio tena la nyuklia'.

Lakini Trump alishutumiwa nyumbani kwa 'kuafikiana kwa mdomo' pasi kufikia makubalino madhubuti kutoka kwa Kim ya kusitisha mipango na matumizi ya nyuklia.
 
Siku ya Jumatatu gazeti la Washington Post limewanukuu maafisa wanaosema Korea kaskazini inaeonekana kuunda kombora moja au amawili ya masafa marefu katika kiwanda cha Sanumdong karibu na mji mkuu Pyongyang.

Kiwanda hicho kiliunda kombora la kwanza la masafa marefu la nchi hiyo lililo na uwezo wa kufika Marekani, gazeti hilo linaongeza.

Kwa mujibu wa Reuters, picha za satelaiti, zinaonyesha magari yakiingia na kutoka kwenye kiwanda hicho , lakini sio kiwango cha ujenzi huo wa makombora.

Hizi sio taarifa za kwanza kuwa Korea kaskazini huenda inaendelea na uundaji wa mpango wake wa silaha, na kutilia shaka athari halisi ya mkutano wa Singapore.

Mwishoni mwa mwezi Juni vyombo vya habari Marekani viliangazia taarifa zinazotokana na uvujaji wa taarifa za ujasusi zinazoashiria kuwa kaskazini ingali inaendeleza shuguli zake za kurutubisha nyuklia katika viwanda vyake miongoni mwa shughuli nyingine.

Wiki iliyopita Mike Pompeo amewaambia Maseneta kuwa viwanda vya Korea kaskazini "vinaendelea kurutubisha kemikali za nyuklia" zinazotumika kuunda silaha.

Chanzo: BBC


from MPEKUZI

Comments