Sheikh awashangaa wanasiasa kugeuka wasemaji wa taasisi za dini

Shekhe wa mkoa wa Dodoma, Mustapha Shaaban amewataka wabunge kufuata shughuli iliyowapeleka bungeni ya kuwawakilisha wananchi wao na kuachana na tabia ya kuwa wasemaji wa dini na madhehebu nchini.

Shekhe Shaaban ametoa kauli hiyo leo Juni 15 kwenye ibada ya Eid  el Fitr iliyofanyika kwenye msikiti wa Ghadafi Jijini Dodoma.

Shekhe Shaaban amesema kuwa kuna baadhi ya wabunge ambao kwa makusudi wameacha majukumu yao yaliyowapeleka bungeni na kuanza kazi ya kuzisemea dini na taasisi ambazo zina wasemaji wake rasmi.
 
Amesema kama kutakuwa na shida au matatizo yoyote yaliyopo kati ya Serikali na madhehebu ya dini nchini kuna wasemaji wake ambao wamewekwa kwa mujibu wa taratibu za dini husika.

"Masuala ya dini tuwaachie viongozi wa dini wenyewe wayasemee kwa kuwa wao ndiyo wahusika na hata kama kuna shida kati yao na Serikali tuwaachie wenyewe na viongozi wa dini wakae na kuzungumza, hii tabia ya kumwacha kila mtu anakuwa msemaji wa dini tutahatarisha amani yetu," amesema Shekhe Shaaban.

Amesema tabia ya kila mtu kuwa msemaji wa dini fulani wakati haijui vizuri ni sawa na kuachia cheche za moto bila kuzizima na madhara yake ni makubwa kwa kuwa zinaweza kuwa moto mkubwa utakaounguza shamba kubwa na kuleta maafa.

Amesema waachiwe wachungaji na maaskofu kusemea masuala ya dini ya Kikristo na mashekhe na Mufti kuzungumzia masuala ya waislamu kwa kuwa ndiyo kazi yao.


from MPEKUZI

Comments