Watuhumiwa 7 Watiwa Mbaroni Dodoma

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Dodoma, Gilles Muroto amemweleza Mkuu wa Mkoa, Dk Binilith Mahenge kuwa jeshi hilo limefanya doria na misako ya wahalifu maeneo ya manispaa ya Dodoma na mji mdogo wa Kibaigwa wilayani Kongwa.

Amesema, katika doria wamemkamata mfanyabiashara mkazi wa Nkuhungu Manispaa ya Dodoma, Josephat Komba (28) akiwa na pikipiki tano aina ya boxer ambazo ni za wizi.

Amewaomba wananchi wa mkoa Dodoma ambao wamepotelewa pikipiki waende kuzitambua.

Amesema wamemkamata Mkazi wa Chang'ombe, manispaa ya Dodoma, Nassoro Masangu (27) aliyetafutwa muda mrefu akidaiwa kuvunja nyumba za watu usiku na kubaka wanawake.

Jeshi hilo pia limekamata watuhumiwa wengine watano kwa unyang'anyi kwa kutumia pikipiki kupora na kutoroka baada ya kufanya matukio hayo. Wamekamatwa wakiwa na pikipiki tatu.

Watuhumiwa hao ni Idd Yusufu (22) mkazi wa Chinangali, Ramadhani Juma (21) wa Hazina, Maneno Jonas (20) wa Chang'ombe, Mohamed Mbinga (22) wa Chinangali na Nzoyi Peter (24) wa Nkuhungu.


from MPEKUZI

Comments