Puto Alilowekewa Tumboni Kigogo IPTL Hatarini Kupasuka

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imeelezwa kuwa hali ya kigogo wa IPTL, Harbinder Sethi inazidi kudhoofika na puto alilowekwa tumboni linaweza kupasuka wakati wowote.

Hayo yamedaiwa leo mahakamani hapo mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi na Wakili wa Sethi, Hajra Mungula ambapo amedai puto hilo linaweza kupasuka na kuhatarisha maisha yake.

Wakili Mungula aliutaka upande wa mashtaka kueleza upelelezi wa kesi hiyo umefikia katika hatua gani kwa sasa kwani Aprili 11,  ilitolewa amri ya mahakama Sethi apelekwe katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa ajili ya matibabu.

“Nashukuru Aprili 18,2018 mshtakiwa alipelekwa Muhimbili, akafanyiwa kipimo cha CT-Scan ya tumboni na alipaswa kupelekwa hospitalini hapo siku inayofuata kwa ajili ya kupatiwa majibu lakini hadi leo hajapelekwa,” amedai.

Baada ya kusikilizwa hoja hizo, Hakimu Shaidi alisema amefurahishwa Sethi kupelekwa hospitali ili apatiwe matibabu na kuamuru apelekwe tena mapema kwa sababu ya afya yake.

Aliamuru upande wa mashtaka kufanya kadiri wawezavyo kukamilisha upelelezi. Kesi imeahirishwa hadi Mei 10,2018 kwa ajili ya kutajwa ili kuangalia kama upelelezi utakuwa umekamilika au la.

Sethi na mfanyabiashara James Rugemarila, wanakabiliwa na mashtaka 12 ya uhujumu uchumi, utakatisha fedha na kuisababisha Serikali hasara ya Dola za Marekani 22, 198,544.60 na Sh bilioni  309.


from MPEKUZI

Comments