Mgogoro Udart, Maxmalipo Watua Bunge

Mgogoro kati ya Kampuni ya Usafiri wa Mabasi yaendayo haraka jijini Dar es Salaam (Udart) na Kampuni ya Maxicom Tanzania (Maxmalipo) umetua bungeni leo baada ya Naibu Spika wa Bunge, Dk. Tulia Ackson kumuagiza Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa kuutolea maelezo wakati akihitimisha hoja ya bajeti ya wizara yake.

Hatua hiyo imekuja baada ya Mbunge wa Kinondoni, Maulid Mtulia (CCM), kuomba mwongozo kwa Naibu Spika kuwa serikali itoe maelezo kuhusu mgogoro huo uliozua usumbufu kwa wananchi wa Jiji la Dar es Salaam kwa muda wa siku tatu sasa.

“Mgogoro huo umesababisha abiria wanaotumia usafiri huo Dar es Salaam kutoka sehemu mbalimbali za jiji kupata usumbufu kwa kukosekana kwa mashine za eletroniki za kutolea tiketi ambayo imesababisha usumbufu lakini pia kuna upotevu wa fedha kwenye upatikanaji wa tiketi hizo jambo lililosababishwa na mgogoro huo wenye harufu ya ufisadi,” amesema.

Hoja hiyo ya Mtulia iliungwa mkono na Mbunge wa Ubungo, Saed Kubenea (Chadema) ambaye aliomba mwongozo kwa Naibu Spika kuwa bunge litumie kanuni ya 47 kusitisha shughuli za bunge na kujadili mgogoro huo kwa dharura.

Akijibu miongozo hiyo Dk. Tulia amesema kwa kuwa miongozo hiyo inahusiana na hoja ya bajeti ya Wizara ya Ujenzi inayohitimishwa leo, waziri husika alitolee maelezo.

“Waziri wakati unahitimisha hoja yako bunge linakuagiza ulitolee maelezo suala hili. Lakini pia haliwezi kusitisha shughuli zake na kulijadili kwa dharura kwa sababu waziri utalitolea maelezo leo baadaye,” amesema Naibu Spika.


from MPEKUZI

Comments