Galis ajitetea kuzimia akiwa kashikilia kitambaa msibani kwa Masogange

Baada ya picha yake inayomuonyesha kazimia huku kashikilia kitambaa mkononi kuibua gumzo jana mitandaoni, msanii wa filamu, Rammy Galis ameeleza kuwa hakuwa amezimia ila alijisikia kuishiwa na nguvu.

Galis alikuwa mmojawapo wa watu waliobeba jeneza la marehemu Agnes Gerald 'Masogange’ katika shughuli za kuuga mwili zilizofanyika viwanja vya Leaders jijini Dar es Salaam jana Jumapili, Aprili 22.

Galis amesema kutokana na kusimama muda mrefu wakati wa shughuli za kuuaga mwili alijikuta akiishiwa nguvu na kuomba msaada kwa wenzie wamuondoe eneo ilipokuwa inafanyikia shughuli hiyo.

"Unajua nilisimama sana tangu tunapofikisha mwili pale viwanjani mpaka watu wanaanza kuaga, nadhani kutokana na hilo nikajikuta naishiwa nguvu, hivyo niliwafahamisha wenzangu kwamba sijisikii vizuri na kuomba waniondoe eneo lile,”

“Hivyo pamoja na wao kuamua kunibeba sio kwamba nilikuwa eti nimepoteza fahamu na ndiyo maana hata kitambaa bado niliweza kukishikilia naomba watu waelewe hivyo na kuacha kunisema kuwa nilikuwa naigiza siwezi kufanya hivyo katika msiba," amesema msanii huyo aliyewahi kutamba kwenye filamu ya Chausiku.

Mbali ya kucheza filamu ya Hukumu na Masogange enzi ya uhai wake,Galis pia alishawahi kuwa na mahusiano ya kimapenzi na marehemu  uliodumu kwa mwaka mmoja (2016-2017).

Masogange aliyefariki Machi 20 mwaka huu akiwa anapatiwa matibabu hospitali ya mama Ngoma, anatarajiwa kuzikwa leo Jumatatu, Aprili 23  jijini Mbeya.


from MPEKUZI

Comments