Mbowe na Viongozi Wenzake Kula Sikukuu ya Pasaka Gerezani

Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Wilbard Mashauri amesema baada ya kusikiliza hoja zilizowasilishwa na upande wa Serikali na utetezi katika kesi inayowakabili viongozi wa Chadema, akiwemo mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe washtakiwa hao wafikishwe mahakamani hapo Aprili 3, 2018.

Amesema siku hiyo washtakiwa watasaini bondi ya Sh20 milioni na wakiwa huru ndipo utaratibu wa kukata rufaa wa upande wa mashtaka utafanyika.
 
 “Nikitoa dhamana wakati washtakiwa hawapo haina maana zoezi zima lisimame.Leo washtakiwa hawajafikishwa mahakamani na nimetoa masharti ya dhamana, hivyo kutoa dhamana na  washtakiwa wakiwa bado hawajasaini ilo zoezi bado halijakamilika.

“Hivyo kwenye hatua ya sasa ni mapema mno kwa upande wa mashtaka kuwasilisha hoja za kukata rufaa wakati bado mchakato haujakamilika.

“Mahakama inatoa remove order waje mahakamani April 3,2018 na wadhamini wao ili waje kukamilisha masharti ya dhamana.”  Amesema Hakimu Mashauri.

Kufuatia uamuzi huo, viongozi hao watakula Sikukuu ya Pasaka wakiwa mahabusu. Sikukuu hiyo inasherehekewa kuanzia kesho hadi Jumatatu.

Awali, Hakimu Mashauri alieleza dhamana kwa washtakiwa hao iko wazi, jambo ambalo lilipingwa na upande wa Serikali.

Washtakiwa hao walitakiwa kila mmoja kuwa na wadhamini wawili ambao watasaini hati ya dhamana ya Sh20 milioni na kuwa na barua kutoka kwa viongozi wao ama wa vijiji au mtaa, ambao watapaswa kuwa na nakala za vitambulisho vyao.

Hakimu alisema kwa asiyeridhika na uamuzi huo ana haki ya kukata rufaa.

Katika mvutano wa kisheria, mmoja wa mawakili wa viongozi hao, Peter Kibatala alipinga taarifa ya rufaa iliyotolewa na wakili wa Serikali.

Kibatala aliiomba mahakama kutekeleza amri yake ya dhamana kwa kuwasainisha washtakiwa bondi ya Sh20 milioni kila mmoja katika tarehe ambayo inaona inafaa na baada ya hapo ndipo ipokee taarifa ya Serikali ya kukata rufaa.

Wakili wa Serikali, Faraja Nchimbi alidai kuwa hilo ni suala la kisheria kwa kuwa taarifa ya rufaa ikishawasilishwa mahakamani na kupokewa, mahakama husika itakuwa imefungwa mikono kuongea chochote kuhusiana na taarifa hiyo kwa maelezo kuwa itakuwa imeingia katika kumbukumbu za mahakama.


from MPEKUZI

Comments