Mpenzi Wangu Ibilisi ( Simulizi ya Kweli) Sehemu ya 04

Mwandishi: Grace Godfrey Rweyemam

Baadaye mchungaji alianza kuyakemea na kuyawashia moto hayo mapepo, yakapiga kelele sana huku yakidai kuwa akiyafukuza yakaondoka mume wake hataweza tena kuishi. Yalidai kuwa kwa yeye kufanya maamuzi ya kwenda kuombewa ni kama kusababisha fedheha kubwa kwa mume wake na hivyo wakuu wake watamuua.

 Yalipiga kelele kwa nguvu yakidai kuungua kisha yakamtoka, nadhani wenye uzoefu wa kukemea mapepo mnanielewa. Nilizungumza na kaka yangu huyu mchungaji akanieleza baadhi ya vitu ambavyo Jovina hakuwa amenieleza kabla.

Baada ya kufunguliwa alimwambia ukweli kuwa mara kadhaa amekuwa akiota kama katika kitanda chao wamelala yeye na mumewe na wanawake hata watatu au wane.

 Alidai hiyo hutokea mara nyingi sana, lakini pia alikiri kuwa licha ya kuwa yeye hufanya tendo la ndoa na mumewe kila siku, lakini siku zote amekuwa ni kama mtu ambaye ana muda mrefu sana hajakutana na mwanaume na hicho kitu kimemsumbua kwa muda mrefu sana. Yaani hali ya mwili wake kutamani mwanaume siku zote iko juu sana.

Siku hiyo baada ya kuombewa alidai hataki tena kwenda nyumbani kwake. “Sitaki tena kumuona mume wangu, simuhitaji tena, sijisikii kuwa naye na hii ni ajabu sana kwani mimi muda wote huwa najihisi kumtamani mume wangu.

Hapa ninawawazia watoto wangu tu, lakini siko tayari tena kuishi nyumba moja na yule shetani tena. Hisia za mapenzi nilizokuwa nazo juu yake hazipo tena na simuoni tena kama mume wangu bali kama adui mkubwa,” Alieleza Jovina huku akisisitiza kutorudi tena nyumbani kwake. Niliwaza ni namna gani kaka yangu huyo mchungaji alitatua hilo, kwani alikuwa bado ni mke wa mtu na ana familia. Pia hapo akili ikaanza kujiuliza ni jinsi gani angerudi nyumbani kwake baada ya kumshambulia mume wake kiasi hicho katika ulimwengu wa roho. 




from MPEKUZI

Comments