Kipindupindu chaua 18 Dodoma

Watu 18 wamepoteza maisha kutokana na ugonjwa wa kipindupindu mkoani Dodoma ndani ya miezi minne huku zaidi ya watu 470 wakiugua ndani ya muda huo.

Mganga Mkuu wa Mkoa huo, Dk. James Kiologwe, alisema jana kuwa ugonjwa huo tangu uingie Dodoma Oktoba, mwaka jana, hadi sasa umesababisha vifo hivyo na idadi hiyo ya wagonjwa.

Alisema wagonjwa wengi wanatoka katika  wilaya za Mpwapwa na Chamwino na miongoni mwa sababu za kuenea kwa ugonjwa huo ni unywaji wa maji ya kwenye madimbwi ambayo si safi na salama.

Mganga mkuu huyo alisema ugonjwa huo ulianza  Oktoba, mwaka jana, katika wilaya zote za mkoa wa Dodoma lakini zaidi katika wilaya hizo mbili.

“Kuna wakati ulipungua, lakini umerudi tena na umekuja sana kwa kasi mwezi huu wa pili,” alisema.

Aidha, Dk. Kiologwe alisema hadi juzi kulikuwa na wagonjwa wapya 26 na 22 kati yao  waliruhusiwa kurudi nyumbani na wanatoka Mpwapwa na Chamwino.

Kuhusu hatua zilizochukuliwa, Dk. Kiologwe alisema jitihada zinaendelea kukabiliana na ugonjwa huo kwa kugawa ‘Water Guard’ vidogo 250,000 kwa ajili ya  kusafisha maji na kuweka  katika vyanzo vya maji.

Aliwataka wakazi wa mkoa huo kuhakikisha wanachemsha maji ya kunywa na kuzingatia kanuni zote za usafi, ili kuepukana na ugonjwa huo.


from MPEKUZI

Comments