Rais Magufuli Atoa Maagizo Mazito kwa Kamishina wq Uhamiaji

 Rais John Magufuli ameitaka Idara ya Uhamiaji kuhakikisha inapambana na wahamiaji haramu pasipo kumwogopa mtu.

Amemwagiza Kamishna wa Uhamiaji, Dk Anna Makakala kuwachukulia hatua kali watumishi wake watakaoshindwa kutekeleza wajibu wao ipasavyo.

Dk Magufuli akizungumza leo Jumatano Januari 31,2018 akizindua hati ya kusafiria ya kielektroniki jijini Dar es Salaam, amesema utambuzi wa wananchi wanaoishi bila vibali na wenye vibali vilivyoisha ni muhimu.

Amesema uhamiaji ina jukumu kubwa katika kutekeleza hayo.

"Haiwezekani wahamiaji haramu wanakamatwa Mbeya halafu wamepita Kilimanjaro, Manyara. Kamishna (Dk Makakala) ifike mahali unapoona hili washushe vyeo, mwondoe nyota moja ili wajue wajibu wao," ameagiza Rais Magufuli.

Amesema awali Uhamiaji iligubikwa na matatizo yakiwamo ya utoaji hovyo wa vibali vya uraia, hata kwa watu ambao walikuwa hawana sifa.

"Kuna raia wengi walipata uraia bila sifa na wapo waliopata uraia na vyeo vya juu kabisa serikalini wakati  si raia," amesema.

Dk Magufuli amesema hiyo ndiyo sababu iliyofanya akamteua Dk Makakala kuwa Kamishna. "Wanawake ni waaminifu sana na ameanza kutatua matatizo haya."

Baadhi ya viongozi waliohudhuria uzinduzi huo ni Rais wa Zanzibar, Ali Mohamed Shein; Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan;  na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.

Wengine ni marais wastaafu Amani Abeid Karume na Ali Hassan Mwinyi; Jaji Mkuu, Profesa Ibrahim Juma; na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Ali Iddi.

Pia, viongozi wa Serikali, Bunge, Baraza la Wawakilishi, wa dini, wanasiasa, na mabalozi wanaoziwakilisha nchi zao Tanzania.


from MPEKUZI

Comments