Mkurugenzi halmashauri Ngara ahimiza michango shuleni Licha ya Serikali Kuzuia

Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ngara, Aidan Bahama amewaomba wadau mbalimbali kuchangia elimu wilayani humo licha ya Serikali kuzuia michango shuleni.
 
Bahama ametoa kauli hiyo jana Januari 25, mwaka 2018 wakati akizungumza na wakuu wa shule za sekondari, msingi, wenyeviti wa bodi na maofisa wa elimu katika kikao cha utendaji.
 
Amesema baada ya tamko la Rais John Magufuli la kupiga marufuku michango shuleni ili kutekeleza mpango wa elimu bure, viongozi hao wanapaswa kusimamia agizo hilo licha ya kuwepo kwa changamoto katika sekta ya elimu.
 
Amesema wadau wa maendeleo ya elimu wakichangia fedha wataweza kupunguza  uhaba wa vyumba vya madarasa, matundu ya vyoo, madawati ,nyumba za walimu na mahitaji mengineyo.
 
 “Hatumzuii mwenye nia ya kuchangia maendeleo ya shule lakini zifuatwe taratibu kwa kuhakikisha kuwa mwalimu hahusiki kushika fedha hizo. Mwalimu abaki kufundisha wanafunzi,” amesema.
 
Amesema shule nyingi wilayani humo zimesajili wanafunzi wengi, baadhi darasa moja lina wanafunzi zaidi ya 120.
 
Amesema shirika la Swash limejitolea Sh1.2bilioni kwa ajili ya kujenga vyoo katika baadhi ya shule za msingi wilayani humo.
 
Ofisa elimu kata ya Muganza, Mohamed Namtimba amesema baadhi ya shule za msingi na sekondari zitaathirika baada ya kusitishwa kwa michango kwa maelezo kuwa michango hiyo ilikuwa ikitumika kulipa walinzi na kununua chakula kwa ajili ya wanafunzi.


from MPEKUZI

Comments