Freeman Mbowe na Wenzake Wagonga Mwamba Mahakamani


Mahakama Kuu divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi imetupilia mbali mapingamizi  yaliyotolewa na upande wa utetezi katika kesi ya ugaidi inayomkabili mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na wenzake watatu na kupokea hati ya ukamataji mali.

Mbowe na wenzake hao, Halfan Bwire, Adamu Kasekwa na Mohamed Ling’wenya wanakabiliwa na kesi hiyo inayosikilizwa na Jaji Joachim Tiganga.

Uamuzi huo unahusu mapingamizi mawili ya mawakili wa utetezi katika kesi hiyo ambayo ni orodha ya vielelezo na mnyororo wa utunzaji vielelezo.

Akitoa uamuzo huo, Jaji Tiganga amesema amepokea ukurasa na kwanza ya nyaraka hiyo na kutopokea ukurasa wake wa pili, kwa kuwa una mashaka.

“Kuna hoja kwamba vitu vimeorodheshwa na kwamba kuna sahihi ya polisi haina tarehe kuonesha iliwekwa tarehe ngapi, katika hali hiyo mahakama inaona mapungufu yako wazi kwenye kielelezo hiki. Mapungufu hayo yanaleta mashaka na yanakuwa resoved kwenye favor ya mshtakiwa, ikumbukwe kielelezo kina page (kurasa) mbili kwa maana ya kwanza imesainiwa na mashahidi wote na ya pili haijasainiwa na haijawekwa tarehe, mahakama inapokea page ya kwa maana inaachana na page ya pili,” amesema Jaji Tiganga.

Jaji Tiganga alitoa uamuzi huo, baada ya mawakili wa utetezi jana kupinga upokelewaji wa nyaraka hiyo, pamoja na mambo mengine, walidai ukurasa wa pili umeingizwa kinyemela, kwa kuwa haikusainiwa na mashahidi walioshuhudia zoezi la ukamataji mali, pamoja na mshtakiwa mwenyewe, bali ina saini ya shahidi aliyeiomba kuitoa kama kilelezo bila ya kuwa na tarehe iliyowekwa.

Mapingamizi hayo yaliibuka baada ya shahidi wa nane wa Jamhuri, SP Jumanne Malangahe, kuiomba mahakama hiyo ipokee hati ya ukamataji mali zinazodaiwa kuwa za Hassan, kama kielelezo cha upande wa mashtaka, akidai alihusika katika uandaaji wake baada ya kufanya upekuzi na kukamata mali za mshtakiwa huyo, tarehe 10 Agosti 2020, nyumbani kwake maeneo ya Yombo Kilakala, Dar es Salaam.

Kuhusu mapingamizi mengine, Jaji Tiganga amesema, ameyatupa kwa kuwa hayana mashiko kisheria.

Kuhusu mapingamizi yaliyodai nyaraka hiyo haina uwezo wa kupokelewa kisheria, pamoja na kutokuwa na uhusiano ikidaiwa kifungu cha sheria iliyotumika katika kuiandaa hakijatamkwa, Jaji Tiganga amelitupa akisema suala hilo haliathiri upokelewaji wa hati hiyo ya ukamataji mali.

“Uzito wa kuto-cite (tamka) kifungu cha sheria inatibika, basi katika mazingira hayo ambayo ni serious kwenye mazingira ya nyaraka kama hii ni lazima na yenyewe inatibika, basi hoja hiyo ya kwanza imelenga bekenye long citation naiondoa kwa sababu nilizoeleza,” amesema Jaji Tiganga.

Akitoa uamuzi dhidi ya pingamizi lililodai hakuna ushahidi unaonesha shahidi aliyeomba kuitoa nyaraka hiyo, alifanya upekuzi nyumbani kwa mshtakiwa huyo, Jaji Tiganga amelitupa akisema, SP Malangahe alitoa ushahidi huo alipodai alihusika katika ukamataji wa mali, zilizopatikana nyumbani kwake Hassan, kisha akamsainisha katika hati ya ukamataji mali.

Katika pingamizi lililodai kuwa jina lililoandikwa katika hati hiyo ya ukamataji mali kuwa sio la mshtakiwa, ambapo liliandikwa Halifan Bwire Hassan, badala ya Halfan Bwire Hassan, Jaji Tiganga ameliweka kiporo akisema litajadiliwa baadae kwa kuwa lina ubishi na haliwezi kuathiri upokelewaji wa nyaraka hiyo




from MPEKUZI

Comments