Marekani Yajipanga Kukabiliana na Virusi Vya Corona

Wakati Marekani ikiwa na kesi sitini za maambukizi ya virusi vya Covid-19, rais wa nchi hiyo Donald Trump, katika mkutano na waandishi wa habari amehakikisha kwamba nchi yake iko tayari kukabiliana na ugonjwa huo.

Mbele ya waandishi wa habari waliokusanyika katika Ikulu ya White House, rais wa Marekani ametaja hatua za tahadhari ambazo tayari zimechukuliwa kama vile marufuku ya kuingia nchini Marekani kwa wasafiri ambao sio raia wa nchi hiyo wanaotokea China na ukaguzi wa kutosha kwenye viwanja vya ndege. 

Amebaini kwamba, viongozi wa nchi hiyo wako tayari kushughulikia hali yoyote ile itakayojitokeza.

"Tuko tayari kabisa, kwa nia na tunafanya kazi, huu ndio utaratibu tunaotumia. Tuko tayari kwa chochote, hata iwapo kutatokea janga kubwa, lakini kwa kweli sidhani kama tutafika hapo.

Tumewazuia wasafiri kutoka China kutoingia nchini Marekani. 

"Tunafuatilia kwa karibu wale wanaotokea katika maeneo mengine yaliyoathirika. Tumewaweka karantini wale ambao wameathirika au wanadalili za virusi vya Covid-19. 

"Tunafanya kazi kwa kupata chanjo yenye nguvu zaidi. Hali imedhibitiwa. Inawezekana kwamba virusi hivyo bado vinaendelea kuenea, au la ... Bado tunafuatilia hali hiyo. Lakini kwa vyovyote vile, tuko tayari, " ameongeza Donald Trump.

Rais wa Marekani amewatolea wito raia wake kutoka kuwa na wasiwasi, akibaini kwamba hata magonjwa mengine ya kawaida husababisha vifo.

"Homa huua kati ya watu 25,000 na 69,000 katika nchi yetu kila mwaka. Mafua vile vile yanasumbua watu!! Wakati kwa sasa, wagonjwa wa Corona ambao tunao hapa nchini wanaendelea vizuri. "

Donald Trump amemteua Makamu wake Mike Pence kuongoza timu itakayosimamia hali hiyo.


from MPEKUZI

Comments