Rufaa Kesi ya Kupinga Wakurugenzi Kusimamia Uchaguzi Yaanza Kusikilizwa

Mahakama ya Rufani imeanza kusikiliza rufaa iliyokatwa na Serikali, yenye mlengo wa kupinga uamuzi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, iliyobatilisha sheria inayowapa mamlaka Wakurugenzi wa Halmashauri kusimamia Uchaguzi Mkuu.

Kesi hiyo namba 6 ya mwaka 2018 ilifunguliwa na watetezi na wanaharakati wa haki za binadamu na demokrasia kwa kushirikiana na vyama vya siasa vilivyowakilishwa na mwanachama wa CHADEMA, Bob Chacha Wangwe dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) na kutolewa maamuzi Mei 10, 2019 na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Atuganile Ngwala.

Kufuatia maamuzi hayo, upande wa Serikali kupitia kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali pamoja na Tume ya Taifa ya Uchaguzi haikuridhishwa na maamuzi ya Mahakama Kuu ndipo walipoamua kukata rufaa.

Rufaa hiyo imesikilizwa  leo na Jaji Augustine Mwarija (kiongozi wa jopo), Stella Mugasha, Richard Mziray, Rehema Mkuye na Jacobs Mwambegele.

Jopo la mawakili wa mjibu rufaa limeongozwa na Wakili Fatuma Karume akishikiana na wakili Mpale Mpokni, Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Dk Nshala Rugemeleza, Jebra Kambole, Fulgence Massawe na  Jeremiah Mtobesya.

Jopo la mawakili wa Serikali limeongozwa na Wakili Mkuu wa Serikali (Solicitor General –SG) Dk. Julius Mashamba huku akisaidiwa na Mawakili wengine 9 wa Serikali.

Katika hukumu yake, Mahakama Kuu ilikubaliana na hoja za Wangwe kupitia kwa wakili wake, Karume na ikisema kuwa kifungu hicho ni kinyume cha Katiba ya Nchi, kwani kinakinzana na matakwa ya Katiba inayotaka Tume ya Uchaguzi iwe huru.

Pia mahakama hiyo ilibatilisha kifungu cha 7 (3) cha sheria hiyo ya Uchaguzi, kinachoipa Nec mamlaka ya kumteua mtu yeyote miongoni mwa watumishi wa umma, kuwa msimamizi wa uchaguzi kwa niaba yake.

Mahakama hiyo ilisema kuwa kifungu hicho hakijabainisha ni namna gani kinampa ulinzi kuhakikisha kuwa anatekeleza majukumu yake kwa uhuru.

Wakati wa usikilizwaji wa rufaa hiyo, Serikali imedai kuwa Mahakama Kuu ilikosea kutamka kwamba vifungu hivyo vinakinzana na Katiba kwa kuzingatia ibara ya 74(14), kwa kuwa ibara hiyo haihusiani na nafuu ambazo mdai alikuwa akiziomba.

Pia imedai kuwa Mahakama Kuu ilikosea kwa kushindwa kutathimini makatazo chini ya Ibara ya 74(14) ya Katiba na ulinzi unaotolewa na Sheria ya Taifa ya Uchaguzi na kanuni zake, Sheria ya Utumishi wa Umma na kanuni zake na sheria nyinginezo zinazohusiana na uendeshaji wa uchaguzi.

Hivyo wameiomba Mahakama ya Rufani ikubaliane na hoja za rufaa hiyo na itengue hukumu ya Mahakama Kuu. 

Hata hivyo, jopo la mawakili wa mjibu rufaa kwa upande wake likijibu hoja hizo za Serikali wamedai kuwa uamuzi wa Mahakama Kuu ni Sahihi na kusisitiza kuwa vifungu hivyo vinakinzana na katika kwa kuwa vinajenga mazingira ya uchaguzi usio huru.

Hivyo wameiomba mahakama hiyo itupilie mbali rufaa hiyo wakidai kuwa haina mashiko na ikubaliane na hukumu ya Mahakama Kuu iendelee kusimama.


from MPEKUZI

Comments