Aliyekuwa Mkurugenzi Jiji la Arusha na wenzake kizimbani kwa uhujumu uchumi


Aliyekuwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Arusha, Dk John Pima na wenzake wanne wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha wakikabiliwa na makosa nane katika kesi mbili za uhujumu uchumi.
 

 Juni 17, 2022 Pima na wenzake watatu Innocent Maduhu (aliyekuwa mchumi wa Jiji), Nuru Ginana (mchumi), Alex Daniel (mchumi), wamefikishwa mbele ya Hakimu Mkazi Bittony Mwakisu na kusomewa mashitaka naneo kwenye kesi mbili tofauti za uhujumu uchumi.

Mbali na washitakiwa hao wanne, mshitakiwa mwingine ni Mariam Mshana ambaye alikuwa Mwekahazina wa Jiji hilo ambaye hakuwepo mahakamani hapo, ambapo upande wa Jamhuri umeiomba mahakama kutoa hati ya wito na kukamatwa kwa mshitakiwa huyo ambaye ni wa pili katika kesi zote.

Jamhuri imewakilishwa na Wakili wa Serikali Mwandamizi Akisa Mhando na Mwendesha Mashtaka wa Takukuru, Hamidu Simbano huku Dk Pima na Maduhu wakiwakilishwa na Wakili Valentine Nyalu.

Katika kesi ya kwanza inawakabili Dk Pima, Mariam, Maduhu na Ginana wanakabiliwa na mashitaka manne ambayo ni ufujaji na ubadhirifu huku makosa mengine yakiwa ni matumizi ya nyaraka kwa lengo la kumdanganya mwajiri.

Aidha washitakiwa hao wataendelea kukaa mahabusu baada ya kushindwa kukidhi masharti ya dhamana ambapo kila mmoja anapaswa kuwa na wadhamini wawili watakaoweka Sh32 milioni au kuwasilisha hati ya mali isiyohamishika yenye thamani hiyo, hadi watakapokamilisha masharti hayo.
Advertisement

Awali, Wakili Mhando aliwasilisha hati ya Mahakama hiyo kupewa mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo.

Mei 24 mwaka huu, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa aliwasimamisha kazi maafisa sita wa Jiji hilo kwa tuhuma mbalimbali ikiwemo matumizi mabaya ya fedha za jiji na tuhuma za kughushi nyaraka.

Watendaji hao walisimamishwa kufuatia tuhuma zilizotolewa na Mbunge wa Arusha Mjini, Mrisho Gambo katika kikao cha watumishi wa jiji kilichokuwa kinaongozwa na Waziri Mkuu Majaliwa.

Kufuatia tuhuma hizo zilizotolewa na mbunge huyo, Waziri Mkuu aliagiza Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) na Takukuru kufuatilia suala hilo.

Kesi hizo zimeahirishwa hadi Julai Mosi mwaka huu ambapo watuhumiwa hao watasomewa maelezo ya awali.



from MPEKUZI

Comments