Mo Dewji Atoa Ya Moyoni.....“sitamvumilia anaenivunjia heshima”


Mfanyabiashara na Mwekezaji wa Klabu ya Simba, Bilionea Mohammed Dewji ‘Mo’ amesema mwaka 2021 hatowavumilia wale wote wanaotoa lugha za matusi na kumvunjia heshima.

Mo ametoa onyo hilo jana kupitia ujumbe wake mrefu wa kufunga mwaka 2020 aliouchapisha kwenye ukurasa wake wa Instagram.

“Azimio langu kwa mwaka ujao humu mtandaoni ni kutovumilia wale wenye lugha za matusi na kunivunjia heshima mimi binafsi.

“Nitalazimika, japo kwa shingo upande na moyo mzito sana, kuwa-block, ku-report na ikibidi, kuchukua hatua za kisheria. Naamini kutumia lugha ya matusi na kudhalilisha dhidi ya mtu katika hadhara si ustaarabu wetu Watanzania, si maadili ya dini zetu na si uungwana pia.

“Sote tuna maisha nje ya mtandaoni. Wengi wetu ni wazazi, tunao pia wazazi, wategemezi na watu wengine muhimu kwetu ambao tunawaheshimu, wanatuheshimu na wana matarajio juu yetu,” amesema Mo na kuongeza kuwa;

“Haipendezi kuwakwaza na kuwaumiza hao wanaotuthamini na kutuheshimu kwa figisu za maisha yetu ya mtandaoni.

“Nachukua fursa hii kuwaomba radhi wale wote niliowakwaza mtandaoni katika mwaka huu unaoishia. Nami nimesamehe wale wote ambao walinikwanza kwa namna moja au nyingine,” amesema Mo.

Aidha, kuhusu Klabu ya Simba, Mo amesema; “Tunapomaliza mwaka, nawashukuru wote humu mtandaoni kwa kunikosoa, kunijenga na kunishauri mengi mimi binafsi na klabu yetu ya Simba.

“Mawazo yenu, michango yenu na matani yenu yamenifanya kufurahia uwepo wangu humu mtandaoni.

“Nawashukuru kwa daima kusimama nami katika nyakati zote na majira yote. Iwe heri, iwe shari, mmenionyesha upendo usio kifani.

“Naahidi kuendelea kuwa mtumiaji mwaminifu, mtiifu na mvumilivu wa mtandao huu mwakani,” amesema MO.


from MPEKUZI

Comments