Jumla ya Shilingi Milioni 219,808,000 Zatolewa kwa Walengwa wa TASAF Busega


 Jumla ya kaya 3,065 Wilayani Busega zimefaidika na mpango wa kunususru kaya masikini TASAF III kipindi cha pili, huku jumla ya shilingi milioni 219,808,000 zikitolewa na serikali kwaajili ya malipo ya kwanza ya awamu ya tatu kipindi cha pili, hayo yamebainishwa na mratibu wa TASAF Wilaya ya Busega, Bi. Wema Mmari.

Mpango wa TASAF awamu ya tatu kipindi cha pili, umetekeleza malipo ya kwanza Wilayani Busega kwa walengwa kulipwa fedha ambapo malipo yamefanyika kuanzia tarehe 23 hadi 25 Septemba, 2020. Malipo hayo yamefanyika huku walengwa wakitoa ushuhuda na kuishukuru serikali kwa utekelezaji wa kipindi cha pili wa TASAF III.

Awali mratibu wa TASAF Wilaya ya Busega Bi. Wema Mmari alisema malipo hayo yamefanyika kwa kaya lengwa zote ambazo zilifanyiwa uhakiki katika zoezi lililofanyika mapema mwezi Julai mwaka huu. Malipo ya kwanza ya TASAF III kipindi cha pili yamejumuisha malipo ya mwezi Julai hadi Oktoba mwaka 2020.

Jumla vijiji 41 kati ya 59 vilivyopo kwenye mpango wa TASAF Wilayani Busega vimefaidika na mradi wa TASAF III kipindi cha pili, huku walengwa wakiaswa kutumia fedha hizo kwaajili ya shughuli za maendeleo ili kuondokana na umasikini.

Sehemu ya walengwa wameishukuru na kuipongeza serikali kwa kuendelea kujali kaya masikini kwani kwa kupitia TASAF kaya nyingi zimepiga hatua kiuchumi. Baadhi yao wamejikita katika shughuli za ufugaji, kilimo, na kununua mahitaji ya vifaa vya shule kwa watoto.



from MPEKUZI

Comments