Wafanyabiashara Manyara Tumieni Fursa ya Michezo kutangaza biashara zenu

Na John Walter-Manyara
Wafanyabishara mkoani Manyara wametakiwa kutumia fursa ya michezo katika kuutangaza mkoa wa Manyara na  biashara zao.

Hayo yameelezwa na Mkuu wa Mkoa wa Manyara Joseph Mkirikiti  leo Agosti 24,2020, wakati akizungumza na wafanyabiashara  mkoani hapo katika kikao kilichofanyika  mjini Babati.
 
Amesema Mashindano ya ngumi Kitaifa mwaka huu yatafanyika mkoani humo kuanzia septemba 6-12 hivyo ni fursa kwa wafanyabiashara wa mkoa wa Manyara kujitokeza kudhamini na kutangaza biashara zao kupitia mashandano hayo makubwa yanayotarajiwa kuhudhuriwa na mamia ya watu kutoka kote nchini.

Aidha Mkirikiti ameitaka Halmashauri ya mji wa Babati,  iharakishe ujenzi wa uwanja wa Michezo Kwaraa unaoendelea kujengwa kwa sasa kwa vibanda vya biashara  kuzunguka uwanja huo.

Amesema kukamilika kwa uwanja huo utafungua fursa ya shughuli za kimichezo na burudani mbalimbali kufanyika katika uwanja huo jambo ambalo litaongeza ukusanyaji wa mapato katika Halmashauri ya mji  na mkoa kwa ujumla.

Kwa upande mwingine amelitaka Shirika la Umeme mkoani humo kuhakikisha wanauwaunganishia umeme wananchi pindi wanapohitaji na kuondoa utiritimba uliopo ili wananchi waendelee kutumia nishati hiyo katika biashara zao.

Mwenyekiti  chama cha wafanyabiashara, Viwanda na Kilimo (TCCIA) mkoa wa Manyara  Stanley Mchome, amesema Wanaridhishwa na utendaji wa awamu ya tano huku akiomba ushirikiano kati ya sekta binafsi na serikali uendelee


from MPEKUZI

Comments