Kamishna CP Liberatus Sabas Awasili Mkoani Songwe Kufuatia Mauaji Ya Mtu Mmoja Yaliosababishwa Na Wafuasi Wa CHADEMA

Mtu mmoja amefariki dunia na wengine watatu kujeruhiwa ambao wanadaiwa kuwa ni makada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) baada ya kutokea vurugu za kisiasa katika mji wa Tunduma mkoani Songwe.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Songwe, George Kyando, akizungumza jana alimtaja aliyeuawa kuwa ni Braiton Mollel.

Waliojeruhiwa katika vurugu hizo zilizotokea kati ya wafuasi wa CCM na Chama cha Demokrsia na Maendeleo (CHADEMA) kuwa ni Elisha Mwaniemba, Fransis Simumba na Mtendaji wa Kata ya Mwaka Kati ambaye alidai jina lake halijapatikana.

Majeruhi Mwaniemba hali ni mbaya na amelazwa katika Hospitali ya Rufani Mbeya.

Kamanda Kyando alisema kufuatia tukio hilo watu 14, wakiwamo viongozi wa vyama vya siasa wamekamatwa kwa tuhuma za mauaji ya kada huyo wa CCM.

Naye Kamishna wa Operesheni na Mafunzo ya Jeshi la Polisi, Liberatus Sabas, ambaye yupo mkoani Songwe kwa ziara, ameagiza kukamatwa wote waliohusika iwe kwa kutamka, kupanga au kutenda katika tukio la mauaji ya Mollel.

Mollel aliyekuwa katika kitengo cha vijana wanaosaidia viongozi na Itifaki (UV-CCM), aliuawa kwa kushambuliwa na kundi la vijana waliovamia Ofisi za Mtendaji wa Kata ya Mwaka Kati Mjini Tunduma wakipinga kuenguliwa kwa mgombea wao baada ya kukosa sifa kugombea udiwani wa kata hiyo.

Alisema licha ya tukio hilo kufanywa katika mazingira ya kisiasa, lakini ni tukio la kihalifu.
 
Kamishna Sabas alivitaka vyama vya siasa nchini kuhakikisha vinafuata taratibu na miongozo iliyotolewa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), ikiwamo kuheshimu sheria.


from MPEKUZI

Comments