Waziri Wa Kilimo Japhet Hasunga Awasilisha TAKUKURU Ripoti Ya Ukaguzi Wa Vyama Vya Ushirika Yenye Ubadhilifu Wa Zaidi Ya Bilioni 124

Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo-Dodoma
Katika mwaka wa fedha wa 2018/19 Serikali ilitoa maagizo kwa Shirika la COASCO kukagua Vyama vya Ushirika vyote. Mpaka tarehe 30 Juni, 2019 Vyama vya Ushirika vilivyosajiliwa vilikuwa 11,410. Kati ya Vyama hivyo, Vyama hai ni 6,463; Vyama Sinzia ni 2,844 na Vyama ambavyo havipatikani 2,103.

Kutokana na maagizo hayo, hadi kufikia tarehe 30 Juni, 2019 COASCO ilikagua Vyama vya Ushirika vipatavyo 4,413 sawa na asilimia 102.63 ya Lengo la Serikali la kukagua Vyama 4,300.

Katika vyama hivyo 4,413 vilivyokaguliwa, vyama 303 (6.87%) vilipata Hati inayoridhisha, vyama 2,378 (53.89%) vilipata Hati yenye shaka, vyama 879 (19.92%) vilipata Hati isiyoridhisha na vyama 853 (19.32%) vilipata Hati mbaya.

Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga (Mb) ametoa takwimu hizo wakati akizungumza na waandishi wa habari wakati wa hafla ya kumkabidhi Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Brigedia Jenerali John Mbung’o ya muhtasari wa uchambuzi wa ukaguzi wa vyama vya Ushirika uliofanywa na Shirika la Ukaguzi wa Vyama vya Ushirika COASCO katika mwaka wa fedha wa 2018/2019 iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Wizara ya Kilimo katika mji wa serikali Mtumba Jijini Dodoma.

Waziri Hasunga alisema kuwa Kati ya Vyama Vikuu 38,Vyama 4 vilipata Hati Safi, vyama 22 vilipata Hati yenye shaka, 9 vilipata hati isiyoridhisha na 3 hati mbaya. Vyama hivyo Vikuu 3 vilivyopata HATI MBAYA inayohusisha hoja zenye viashiria vya ubadhirifu wenye Jumla ya shillingi 856,357,955 kwa RUNALI, SCCULT 4,878,662,431 na KYECU kwa kukosekana kwa hati za kuhesabu mali za kudumu mwisho wa mwaka.

Alisema kuwa Chama Kilele (Shirikisho-TFC) kimepata Hati Isiyoridhisha ambayo inajumuisha fedha benki zisizofanyiwa malinganisho na pia kutooneshwa katika taarifa za fedha kiasi cha shilling 1,538,726,787

Kati ya Vyama vya Ushirika wa Mazao (AMCOS)  2,710 vilivyokaguliwa, vyama 15 vilipata Hati Safi, 1347 Hati yenye Shaka, 599 Hati Isiyoridhisha na vyama 749 vilipata Hati Mbaya.  Matatizo makuu katika vyama hivyo vya AMCOS ni kushindwa kuandika vitabu vya hesabu, malipo mengi kutokuwa na vielelezo vya malipo, mifumo dhaifu ya udhibiti wa makusanyo na mauzo ya mazao, kukosekana kwa daftari la mali za vyama na watendaji wa vyama kutokuwa na weledi wa kuandika vitabu na taarifa za fedha za vyama. Kati ya SACCOS 1,448 SACCOS 261 zilipata Hati Safi, 887 yenye Shaka, 218 Isiyoridhisha na 82 Hati Mbaya.

Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga ameyataja matatizo makuu ya SACCOS nyingi kuwa ni kushindwa kuandika vitabu ipasavyo, marejesho ya mikopo ya wanachama kutofanyika kwa wakati, baadhi ya waajiri kuchelewesha kuwasilisha makato ya wanachama kwa SACCOS, madeni makubwa yanayothiri utendaji wa SACCOS, miamala ya benki kutofanyiwa malinganisho na baadhi ya miamala kuwa na ubadhirifu.

Mhe Hasunga amesema kuwa katika ukaguzi wa kawaida kwa mwaka 2018/2019 Fedha zenye Mashaka (nia ovu) ni Tsh 87,694,976,970, Hasara iliyotengenzwa kwa uzembe ni Tsh 22,861,038,064 huku Wizi/Ubadhirifu ikiwa ni Tsh 2,840,752,866 ambapo jumla ya fedha hizo ni Tsh 113,396,767,900

Pia alisema kuwa katika ukaguzi maalumu kwa mwaka huo wa 2018/2019 Fedha zenye Mashaka (nia ovu) ni Tsh 6,266,796,345.63, Hasara iliyotengenzwa kwa uzembe ni Tsh 2,634,438,512.00 wakati Wizi/Ubadhirifu ni Tsh 1,755,248,116.00 ambapo jumla yake ni Tsh 10,656,482,973.63

Amesema kuwa jumla kuu ya fedha za ukaguzi wa kawaida na ukaguzi maalumu ni kwa mwaka wa fedha 2018/2019 mi Tsh 124,053,250,874.00

Alisema kuwa mbali na vyama hivyo vilivyokaguliwa, vipo vyama 682 vilikataa kuwasilisha vitabu kwa ajili ya ukaguzi na kuongeza kuwa Kati ya vyama 853 vyenye Hati Mbaya, vipo vyama vyenye viashiria vya ubadhirifu wa fedha na mali vipatavyo 130 na vyama vyenye matatizo mbalimbali ya uongozi na utendaji 723.

Pia, Amesema kuwa kwa mujibu wa taarifa hiyo aliyoikabidhi TAKUKURU baadhi ya Waajiri wameonekana kuchelewesha michango ya Wanachama baada ya makato na kuathiri uhai wa vyama katika kutoa mikopo kwa Wanachama.


from MPEKUZI

Comments