Jeshi la Polisi Lazuia Mkutano wa Mchungaji Peter Msigwa

Jeshi la Polisi mkoani Iringa, limezuia mkutano wa Mbunge wa Iringa Mjini (Chadema), Mchungaji Peter Msigwa, kwa madai ya kutokuwapo kwa askari wa kutosha wa kulinda mkutano huo.

Taarifa za kuzuiwa kwa mkutano huo zilisambaa kwenye mitandao ya kijamii, ikionyesha barua ya zuio kutoka polisi. Mkutano huo ulikuwa ufanyike katika viwanja vya Mwembetogwa.

Kamanda wa Polisi Mkoani Iringa, Juma Bwire, alisema marufuku hiyo ilitokana na kutokuwapo kwa askari wa kutosha kwa kuwa wako kwenye usimamizi wa mitihani ya kidato cha nne, kidato cha pili na darasa la nne pamoja na kuwapo kwa taarifa za kiintelijensia juu ya kutokea vurugu na kusababisha uvunjifu wa amani.

Kamanda huyo amesema sababu nyingine ni dalili za kuanza kampeni mapema za kuelekea uchaguzi wa Serikali za Mitaa kabla ya kalenda ya kampeni kuanza.

Kamanda huyo amebainisha kuwa sababu nyingine ni barua ya mkutano huo kutoweka wazi dhumuni la mkutano ikiwa ni kinyume cha kifungu cha 43(1)(b) cha Sheria ya Polisi na Polisi wasaidizi sura 322 kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.

 
Akizungumzia kuhusu kuzuiwa mikutano yake, Msigwa alisema hiyo ni kinyume cha sheria kwa kuwa Mbunge hutakiwa kutoa taarifa ili kuhakikisha usalama wa mikutano yake na si kuomba ruhusa kwa jeshi hilo.

"Mimi ni mbunge na ile ndiyo kazi yangu. Sasa kazi yao ni kulinda mikutano yangu ili pasitokee vurugu na si kuzuia." alisema Msigwa.


from MPEKUZI

Comments