Uturuki yamuonya vikali mbabe wa kivita wa Libya Jeneral Khalifa Haftar

Uturuki imesema kuwa vikosi vya kiongozi wa Libya Khalifa Haftar ”vitalengwa” ikiwa hawatawaachia huru haraka raia sita wa Uturuki. 

Vikosi vya Jenerali Haftar vilisema siku ya Ijumaa kuwa vitashambulia maslahi ya Uturuki kwa kuwa taifa hilo linaunga mkono serikali ya Libya inayoungwa mkono na jumuia ya kimataifa.

Pia walidai kuwa waliharibu ndege isiyo na rubani ya Uturuki kwenye anga la Tripoli.

Libya imekumbwa na machafuko na mgawanyiko tangu kuondolewa madarakani na kuuawa kwa aliyekuwa kiongozi wa taifa hilo, Muammar Gaddafi mwaka 2011.

Jenerali Haftar alianza mashambulizi dhidi ya serikali inayotambuliwa na jumuia ya kimataifa,(GNA) inayoongozwa na waziri mkuu Fayez al-Sarraj, mwezi Aprili.

Uturuki inaunga mkono GNA, inapeleka ndege zisizo na rubani, silaha na magari kwa ajili ya kusaidia juhudi za serikali kupambana na vikosi vya Jenerali Haftar, ambavyo vinadhibiti sehemu kubwa ya mashariki na kusini mwa Libya.

Jenerali Haftar kutoka jeshi la taifa la Libya (LNA) amesema atashambulia meli za Uturuki kwenye maji ya Libya na maeneo muhimu ya kibiashara ya Uturuki.

Pia amezuia ndege za kibiashara kutoka Libya kwenda Uturuki.

Mapema siku ya Jumapili, Uturuki ilisema ”italipa kisasi kwa kuchukua hatua kali zaidi” kwa vitisho vyovyote kutoka kwa vikosi vya Jenerali Haftar.

Waziri wa ulinzi wa Uturuki, Huluski Akar ameonya kuwa vikosi vya LNA vya Libya vitalipa mashambulizi yoyote watakayofanya dhidi ya maslahi ya Uturuki.

Uturuki imesema inataka kupunguza mapigano dhidi ya Jenerali Haftar, ambaye anaungwa mkono na Umoja wa falme za kiarabu na Misri.

Siku ya Alhamisi, GNA ilichukua mji muhimu wa Gharyan, mji ambao ni ngome ya vikosi vya bwana Haftar.

Credit:BBC


from MPEKUZI

Comments