Ndugai ataka tamko la serikali kuhusu Watanzania Kupewa Masaa 24 Waondoke Kenya

Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai ameitaka serikali kutoa tamko kufuatia kauli yenye kuashiria ubaguzi aliyoitoa mmoja wa wabunge wa Kenya.

Amesema hayo kufuatia kusambaa kwa video mtandaoni ikimuonesha Mbunge wa Jimbo la Starehe nchini Kenya, Charles Njagua Kanyi 'Jaguar', akitishia usalama wa wageni mbalimbali wanaofanya kazi pamoja na biashara nchini humo.

Leo Jumanne, Juni 25, Mbunge wa Rufiji-CCM, Mohammed Mchengerwa amehoji bungeni juu ya umuhimu wa Serikali kutoa ulinzi kwa Watanzania wanaoishi, kufanya kazi pamoja na biashara nchini Kenya, ndipo Spika Ndugai alipotoa rai hiyo kwa serikali.

"Ninaiomba Serikali kutoa tamko hii leo kufuatia kitendo hiki", amesema Spika Ndugai.

Katika video hiyo inayosambaa kwa kasi, Mbunge Jaguar amesema, "hapa hatuwazungumzii wachina 6, tunawazungumzia mamia ya wageni wanaofanya kazi hapa. Ninaipa serikali masaa 24 kuwaondoa hawa wageni, endapo itashindwa, nikiwa kama mwakilishi wa eneo hili, tutakwenda katika maduka, tutawapiga na kuwafurusha hadi uwanja wa ndege ili warejeshwe walikotoka".

Kauli hiyo ya Jaguar imewalenga zaidi raia wa Tanzania na Uganda, ambao kwa madai yake ndiyo waliochukua fursa zao za kibiashara nchini humo.


from MPEKUZI

Comments