Kisukari (Diabetes Mellitus) : Chanzo, Dalili na Matibabu Yake

Miongoni mwa magonjwa sugu yanayoendelea kuathiri afya za mamilioni ya watu wa nchi nyingi duniani ikiwemo Tanzania ni ugonjwa wa kisukari. 


Ugonjwa huu hutokea pale ambapo tezi kongosho linaposhindwa kutengeneza kichocheo aina ya Insulin au pale mwili unaposhindwa kutumia vizuri kichocheo hicho cha insulin na kusababisha kuongezeka kwa kiwango cha sukari kwenye damu au hyperglycemia.
 
Aina za Kisukari
Kisukari kimeanishwa katika makundi yafuatayo
 
Aina ya kwanza ya Kisukari au Type 1 Diabetes Mellitus
Hii ni aina ya kisukari inayowaathiri zaidi watoto na vijana

Aina hii hutokea iwapo seli maalum zinazotengeneza homoni ya insulin zijulikanazo kama beta cells of Islet of Langerhans katika tezi kongosho zitakosekana au zitaharibika kwa sababu yeyote ile, na hivyo kusababisha ukosefu kabisa au upungufu wa kichocheo hicho kwenye damu.

Mambo yanayoweza kusababisha uharibifu wa seli hizi katika tezi kongosho ni pamoja na kushambuliwa kwa tezi kongosho kunakoweza kufanywa na magonjwa ya kinga ya mwili wa mtu mwenyewe au autoimmune diseases; au kushambuliwa na vyanzo visivyojulikana yaani idiopathic causes.

Kwa vile, uharibifu katika tezi kongosho hupelekea ukosefu wa insulin au hufanya insulin kuzalishwa kwa kiwango kidogo sana, wagonjwa wa aina hii ya kisukari uhitaji kupewa dawa za insulin kwa njia ya sindano kila siku za maisha yao ili waweze kuishi. Ndiyo maana aina hii ya kisukari huitwa pia Kisukari kinachotegemea Insulin au Insulin Dependent Diabetes Mellitus (IDDM)
 
Aina ya pili ya Kisukari au type 2 Diabetes Mellitus
Hii ni aina ya kisukari inayotokea zaidi ukubwani. Aina hii ya kisukari husababishwa na kupungua kwa ufanisi utendaji kazi wa homoni ya insulin.

Hali hii husababishwa na unene uliopitiliza yaani obesity, au hali ya kutofanya mazoezi kabisa (physical inactivity).

Kwa vile, katika aina hii ya kisukari, insulin huzalishwa katika kiwango cha kutosha isipokuwa tatizo lipo kwenye ufanisi wa utendaji kazi wake, wagonjwa wa aina hii ya kisukari hawahitaji kupewa insulin kwa njia ya sindano. Ndiyo maana aina hii hujulikana pia kama kisukari kisichotegemea insulin au Non Insulin Dependent Diabetes Mellitus (NIDDM)
 
Kisukari cha Ujauzito (Gestational DM)
Ni aina ya kisukari kinachotokea pindi kunapokuwa na ongezeko la kiwango cha sukari katika damu (hyperglycemia) wakati wa ujauzito.

 Aina hii ya kisukari huathiri karibu asilimia 2-5 ya mama wajawazito wote ingawa wengi wao hupata nafuu na kupona kabisa mara tu baada ya kujifungua. 

Hata hivyo karibu asilimia 20 mpaka 50 ya mama wajawazito wanaopata aina hii ya kisukari huweza kuendelea nacho hatimaye kuwa aina ya pili ya kisukari au type 2 DM maishani.
 
Kisukari husababishwa na nini?
Visababishi vya kisukari hutofautiana kulingana na aina husika ya kisukari.
  1. Visababishi vya aina ya kwanza ya kisukari: Aina ya kwanza ya kisukari ina uhusiano mkubwa sana na kurithi. Aidha aina hii pia husababishwa na maambukizi ya Coxsackie virus type B4. Visababishi vingine ni pamoja na sumu inayotokana na kemikali za baadhi ya vyakula (food borne chemical toxins), na kwa baadhi ya watoto wachanga maziwa ya ng’ombe yanaweza kuchochea kinga ya mwili wa mtoto kuushambulia mwili wenyewe (autoimmune reaction) na hivyo kupelekea uharibifu katika tezi kongosho.
  2. Visababishi vya aina ya pili ya kisukari: Kwa ujumla aina hii ya kisukari husababishwa zaidi na mfumo wa maisha na matatizo ya kijeneteki. Aidha vitu kama kuongezeka uzito na unene kupita kiasi (obesity) nayo pia huchangia kutokea kwa aina hii ya kisukari. Sababu nyingine ni pamoja na Kuongezeka umri, maisha ya kivivu na kutofanya mazoezi (physical inactivity) na pia ugonjwa wa tezi kongosho (pancreatitis) ambao hufanya insulin inayozalishwa kuwa na ufanisi mbovu au ya kiwango cha chini.
Dalili za Kisukari
  1. Kukojoa mara kwa mara (polyuria)
  2. Mgonjwa kujihisi kiu kikali na kunywa maji kupitiliza (polydipsia)
  3. Mgonjwa kujihisi njaa na kula mara kwa mara (polyphagia)
  4. Kuchoka haraka (easy fatiguability)
  5. Kupungua uzito
  6. Vipele mwilini ambavyo kitaalamu huitwa diabetic dermadromes
  7. Wagonjwa wa kisukari pia huwa katika hatari ya maambukizi katika kibofu cha mkojo, ngozi na kwa wanawake sehemu za siri.
Aidha kuna dalili maalum ambazo hutokea kwa wagonjwa wa kisukari iwapo mgonjwa atapatwa na mojawapo ya madhara (complications) ya ugonjwa huu.  Madhara (complications) haya hujulikana kama Diabetic Ketoacidosis na Hyperosmolar non-ketotic coma. Diabetic Ketoacidosis au kwa kifupi DKA hutokea kwenye aina ya kwanza ya kisukari (type 1 DM), nayo huwa na dalili zifuatazo
  1. Mgonjwa hutoa harufu ya acetone (inafanana kiasi na harufu ya pombe)
  2. Mgonjwa hupumua kwa haraka na kwa nguvu, hali hii huitwa Kussmaul's breathing
  3. Kujihisi kichefuchefu
  4.  Kutapika
  5.  Kujihisi maumivu ya tumbo na
  6.  Kupoteza fahamu.
Hyperosmolar Non-ketotic coma hutokea kwenye kisukari cha aina ya pili (type 2 DM). Hali hii mara nyingi husababishwa na upungufu wa maji mwili (dehydration) na mgonjwa huweza kupoteza fahamu.
 
Vipimo na Uchunguzi

Baada ya vipimo, tunaweza kusema kuwa mtu fulani ana kisukari iwapo
  1. Kiwango cha sukari kwenye damu kipo ≥7mmol/L (sawa na 126mg/L) iwapo kipimo kitafanyika kwa mtu ambaye hajala chakula chochote. Kwa jina jingine kipimo hiki huitwa Fasting Blood Glucose (FBG)
  2.  Kiwango cha sukari kwenye damu kipo ≥ 11.1mmol/L (sawa na 200mg/L) kwa mtu ambaye amelishwa gram 75 za glucose ndani ya masaa mawili. Kipimo hiki pia huitwa Oral Glucose Tolerance Test (OGTT).
  3. Au, iwapo mgonjwa atafanyiwa kipimo kinachoitwa glycoslytated hemoglobin (Hb A1C).
Madhara ya Kisukari
Kisukari huweza kusababisha madhara yafuatayo kwa muhusika iwapo hakitatibiwa inavyopaswa.
  1.  Kuziba kwa mishipa mikubwa ya damu kutokana na kuzungukwa na mafuta (Atherosclerosis)
  2.  Mgonjwa kushindwa kuona vizuri au kushindwa kuona kabisa na kuwa kipofu (diabetic retinopathy)
  3.  Kushindwa kufanya kazi vizuri kwa figo
  4.  Mgonjwa kuhisi ganzi na kupoteza kuhisi mikononi na miguu kwa sababu ya kuharibika kwa neva (diabetic neuropathy)
  5.   Kupungua kwa nguvu za kiume.
  6.  Vidonda (diabetic ulcers) hususani vidoleni. Hali hii wakati mwingine hupelekea mgonjwa kukatwa viungo vyake.
  7.  Mgonjwa kuwa hatarini kupata maambukizi ya vimelea mbalimbali hasa bakteria kutokana na kuharibiwa na kushindwa kufanyakazi vizuri kwa chembe nyeupe za damu (White Blood Cells)
Matibabu
Matibabu ya kisukari hutegemea na aina ya kisukari ingawa kwa ujumla kuna hujumuisha matumizi ya dawa na njia ya kubadilisha mfumo (staili) wa maisha.

Kwa aina ya pili ya kisukari (type 2 DM au NIDDM): Aina hii ya kisukari huweza kutibiwa kwa ama dawa au kubadili mfumo wa maisha au vyote viwili kwa pamoja. Katika kubadili mfumo wa maisha, ni muhimu mgonjwa kutilia maanani na kuwa makini na vitu kama aina ya vyakula anavyokula, na kujitahidi na kuongeza kufanya mazoezi ya mwili ili kuepuka kuongezeka uzito kupita kiasi. Kuhusu aina ya vyakula inashauriwa sana
  1. kupunguza kula vyakula vyenye lijamu (cholesterol) ambayo ni mafuta mabaya yaani kula walau chini ya miligramu 300 za lijamu kwa siku.
  2.  kujitahidi sana kula vyakula vya kujenga mwili (protein) angalau kwa asilimia 10-15. Vyakula hivi ni pamoja na nyama na mboga za majani.
  3. kuwa makini na ulaji wa vyakula vya wanga (carbohydrate). Hakikisha visizidi asilimia 50-60 ya chakula unachokula kwa siku. Yaani visiwe ndiyo chakula kikuu kwa siku.
  4.  kupunguza utumiaji wa chumvi katika chakula.
  5.  Kuacha na kuwa muangalifu kutumia pombe.
Suala la ufanyaji mazoezi ni jambo la muhimu kwa vile mazoezi husaidia sana kupunguza uzito, kuondoa mafuta mwilini yanayopunguza utendaji kazi wa insulin na hivyo kuongeza ufanisi na utendaji wa insulin mwilini.

Hali kadhalika, mgonjwa mwenye aina hii ya kisukari anaweza pia kupewa dawa ambazo atatakiwa kunywa kila siku huku akiendelea kufuata ushauri mwingine kama ilivyoelezwa hapo juu.

Dawa hizo ambazo huitwa pia dawa za kushusha kiwango cha sukari mwilini (Oral Hypoglycemic drugs) ni pamoja na zile za kundi la Biguanides kama vile Metformin, za kundi la Sulphonylureas kwa mfano Glipizide, za kundi la Meglitinides, za kundi la Alpha glucosidase inhibitor, zinazojulikana kama Thiazolidinediones, Incretin-mimetic au za kundi la Dipeptidyl peptidase IV inhibitors kwa mfano sitagliptin

Ifahamike pia kuwa wapo baadhi ya wagonjwa wa aina hii ya pili ya kisukari (Type 2 DM) ambao pamoja na kutumia dawa za kunywa za kushusha sukari na kufuata ushauri wa daktari kuhusu mfumo wao wa maisha bado njia hizo zinaweza zisishushe sukari inavyotakiwa. Katika hali kama hiyo, wagonjwa hawa huweza kudungwa pia sindano za insulin kwa muda ili kushusha kiwango cha sukari.
 
Kwa Aina ya Kwanza ya kisukari (Type 1 DM au IDDM)
Pamoja na kurekebisha aina ya vyakula na mazoezi, wagonjwa hawa huitaji kichocheo cha Insulin ili kudhibiti kiwango cha sukari katika damu.

Dawa za Insulin zimegawanyika katika makundi makuu matatu. Kuna zile zinazofanya kazi kwa muda mfupi (short acting), za muda wa kati (intermediate acting) na zinazofanya kazi kwa muda mrefu (long acting).Kulingana na utendaji wa dawa hizo, mgonjwa anaweza kuelekezwa jinsi ya kujidunga mwenye sindano za insulin nyumbani kwa kufuata maelekezo yafuatayo
  1.  Asubuhi: Mgonjwa hujidunga 2/3 ya insulin nusu saa kabla ya kunywa chai.
  2. Usiku: Mgonjwa hujidunga 1/3 ya insulin nusu saa kabla ya chakula cha usiku.
  3.   Aidha katika hii 2/3 inayotolewa asubuhi, 2/3 yake huwa insulin inayofanya kazi kwa muda wa kati (intermediate acting) na 1/3 ni ile inayofanya kazi haraka (short acting).
  4. Inasisitizwa sana kutojidunga sindano hii bila kupata maelekezo sahihi kwa daktari. Kwa maelekezo zaidi na sahihi ya matibabu kwa kutumia Insulin ni vizuri kuhudhuria kliniki za kisukari, ambazo hupatikana karibu hospitali nyingi hapa nchini.
Matibabu maalum
Matibabu ya hyperosmolar non-ketotic coma (HONKC): Matibabu haya hutolewa hospitali. Mkazo huwekwa katika kusahihisha upungufu wa maji mwilini ambapo mgonjwa hupewa kati ya lita 8 hadi 10 za maji aina ya Normal saline. Aidha, lita kati ya 1 hadi 2 hutolewa katika masaa ya mwanzo tangu mgonjwa kufkia hospitali. Iwapo kuna ugumu katika kusahihisha kiwango cha kisukari mwilini kwa kutumia dawa za kunywa, Insulin inaweza kutolewa.
 
Matibabu ya Diabetic ketoacidosis (DKA): Kama ilivyo kwa hyperosmolar non-ketotic coma, matibabu ya DKA nayo hutolewa hospitali chini ya uangalizi maalum wa madaktari. Hii ni hali ya hatari, ambapo kama isipotibiwa kwa umakini, inaweza kupelkea kifo cha mgonjwa. Jambo la muhimu katika matibau ni kusahihisha upungufu wa maji mwilini kwa kutumia Normal saline, ambapo lita 1-3 hutolewa ndani ya masaa mawili ya mwanzo, kusahihisha kiwango cha potassium kilichopo katika damu na kurekebisha kiwango cha sukari kwenye damu kwa kutumia Insulin.

Credit: Dr Mayala, TanzMed



from MPEKUZI

Comments