TAKUKURU Yazirejesha Sh. Bilioni 14.9 Kutoka Kwa Mafisadi.....Yatangaza Kumsaka Mwanamke Mmoja Ambaye Ametoroka

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) inamtafuta mwanamke mmoja aliyefahamika kwa jina la Magreth Kobelo mkazi wa Kinondoni jijini Dar es salaam, kwa makosa ya utakatishaji fedha na kujipatia mali, kupitia kampuni  iliyokuwa ikifanya kazi bila kulipa kodi.

Akizungumza leo Jumanne Machi 26, jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Kamishna wa Polisi, Athuman Diwani, amesema wakati uchunguzi ukiendelea mtuhumiwa huyo alitoroka nchini.

Amesema mtuhumiwa huyo kwa kutumia fedha ambazo ni zao la ukwepaji kodi alinunua viwanja vitatu vilivyoko ufukweni katika Manispaa ya Temeke na nyumba tatu za kifahari zilizoko Tegeta Manispaa ya Kinondoni.

“Tumeamua kutangaza kutafutwa kwake kabla ya kutaifisha mali alizojipatia kwa rushwa.

“Asiporudi nchini kwenye kesi inayomkabili madhara yake ni makubwa sana kwake binafsi na familia yake kwa kuwa mali zitataifishwa na kurudishwa serikalini kwa mujibu wa sheria,” amesema Kamishna Diwani.

Katika hatua nyingine, Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Kamishna wa Polisi, Athuman Diwani amesema wamefanikiwa kuzirejesha fedha mali ya Uma zaidi ya Sh14.9 bilioni, na kutaifisha nyumba saba na magari manne kutoka kwa mafisadi.

“Kuanzia mwaka 2016 hadi sasa, Takukuru imefanikiwa kurejesha zaidi ya Sh14.9 bilioni na kutaifisha nyumba saba na magari manne kutoka kwa mafisadi.

“Tumeweka zuio la mali ikiwamo akaunti za fedha zaidi ya Sh20 bilioni, nyumba 26, viwanja 47, magari 61 na mashamba 13.”Amesema

Amesema Takukuru ina mamlaka ya kufuata sheria ya kutafuta, kushikilia na kutaifisha mali kupitia tangazo la kutafutwa.


from MPEKUZI

Comments