Rais Magufuli Atoa Zawadi Ya Viwanja Kwa Wachezaji Wote Wa Taifa Stars Pamoja Na Bondia Mwakinyo

Baada ya timu ya taifa ya Tanzania Taifa Stars kuifunga Uganda 3-0 katika mchezo wa kuwania kufuzu kucheza AFCON 2019 na kufuzu kwa mara ya kwanza baada ya miaka 39, Rais Magufuli aliwaita wachezaji Ikulu Dar es Salaam kwa ajili ya kuwapongeza na kuwapa zawadi wachezaji.

Rais Magufuli akiwa na wachezaji hao pamoja na bondia wa kitanzania Hassan Mwakinyo baada ya kumpiga bondia wa Argentina Gonzalez, Rais Magufuli ametangaza kutoa Tsh Bilioni 1 kwa ajili ya maandalizi ya fainali za AFCON U-17 zinazofanyika Tanzania mapema mwezi April.

Pamoja na hayo Rais Magufuli ametoa zawadi ya viwanja kwa wachezaji wote wa Taifa Stars na kuwaagiza wapatiwe viwanja hivyo makao makuu ya nchi Dodoma, mchezaji wa zamani wa Taifa Stars Peter Tino aliyefunga goli la Taifa Stars kucheza AFCON 1980, Rais Magufuli amempa Tsh Milioni 5 baada ya mchezaji huyo kusema kuwa hana cha kufanya kwa sasa.

“Kila mmoja apate kiwanja chake, kama Serikali ilitoa viwanja kwa mabalozi wa nchi nyingine, hatuoni sababu ya mabaloz wa Taifa letu (Taifa Stars na Hassan)kwanini wasipatiwe viwanja. Haiwezekanani baada ya kustaafu wanabaki hawana kitu , lazima tutambue kazi ambayo wameifanya kwa niaba ya nchi yetu ,”amesema Rais Magufuli.

Rais Magufuli amesema anatambua mchezaji wa kimataifa na Nahodha wa Taifa Stars Mbwana Samatta ameondoka nchini jana kurudi kwenye timu yake lakini naye asisahaulike kwenye zawadi ya kiwanja huku akitumia nafasi  kutoa maagizo kwa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kusimamia upatikanaji wa viwanja hivyo.

Kuhusu mchezo wa jana amesema amefurahishwa na uchezaji wa Taifa Stars kwani wamejituma sana uwanjani na ukweli ni kwamba walikuwa wanapiga pasi nzuri .


from MPEKUZI

Comments