Mkurugenzi TAMWA Awasihi Wazazi Kuacha Kuwahamasisha Watoto Kujifelisha Mitihani Kwa Makusudi.

Na Bakari Chijumba,Lindi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Wanahabari  Wanawake Tanzania (TAMWA) Bi Rose Reuben, amewataka wanawake wa Ruangwa kubadilika na waweke juhudi katika kupinga kuishi kwenye maisha ya ukatili wa kijinsia.

Aidha amewataka wazazi kuacha kuwanyima watoto haki ya kupata elimu, kwani ni jukumu la mzazi kumpatia mtoto elimu na si kumshawishi afanye vibaya katika mitihani yake ya mwisho.

Mkurugenzi huyo, ameyasema hayo  Machi 29 March 2019, wakati wa mkutano wa wadau wa kujadili mbinu mkakati ya  kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake na watoto katika ukumbi wa Rutesco uliopo  Ruangwa mjini,katika wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi.

Bi Rose alisema lengo la TAMWA ni kusaidia jamii kuondokana na changamoto za ukatili wa kijinsia hivyo wataendelea kuhakikisha changamoto hizo zinaisha katika jamii ya Ruangwa

"Suala la kupinga ukatili wa kijinsia si la TAMWA pekee yake ni jukumu la kila mwananchi hivyo tusaidiane kubainisha changamoto hizo na sisi tutasimamia kutoa elimu katika kuhakikisha tunatokomeza hizo changamoto"alisema Bi Rose.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Ruangwa, Hashim Mgandilwa, ametoa rai kwa wananchi wa Ruangwa kuacha kuwahamasisha watoto kufanya vibaya katika mitihani yao ya mwisho ya darasa saba na kidato nne kwa makusudi.

Mheshimiwa Mgandilwa  alisema mzazi atakayebainika anafanya jambo la kushawishi mtoto kufeli kwa kisingizo cha kukosa uwezo wa kusomesha atamchukulia hatua za kisheria.

Pia aliwataka wazazi wa Ruangwa kubeba majukumu yao kama wazazi kwa kuwasimamia watoto wao katika mienendo iliyobora na kuwahamasisha watoto hao kufanya vizur katika masomo yao.

Mgandilwa ametoa rai kwa uongozi wa TAMWA kusaidia kutatua changamoto zilizobainishwa na wadau ili kumaliza matatizo yanayowakabili watoto na wanawake.

"Nitoe shukurani za dhati kwa jitihada mnazozifanya TAMWA na nitapenda sana siku mkiniambia nije nizindue bweni mlilojenga kwa ajili ya kusaidia watoto wanaotembea umbali mrefu hasa wa kike" alisema Mgandilwa.

Mjumbe wa mkutuno huo Esha Issa, amesema wanaochangia mmomonyoko wa maadili kwa watoto ni wamama wenyewe kwani wamekuwa ndiyo watu wenye sauti kubwa katika familia na wanaitumia sauti hiyo vibaya.

"Wamama hatutaki watoto wetu wasemwe wakikosea hata ukiletewa mashitaka ya mtoto anafanya uhuni unakuwa mkali utaki kuamini na hata akipata mimba unaishia kusema acha aongeze dunia"alisema na kuongeza;

"Hili ni tatizo sana kwani watoto wetu wanakuwa hawana adabu na wanapata nguvu ya kufanya mambo ya ajabu kwasababu anaona mzazi mwenyewe unafurahia ujinga anaoufanya".

Mjumbe huyo amewashukuru uongozi wa TAMWA na  aliuomba uongozi huo kutoa elimu ya madhara ya unyanyasaji wa kijinsia kwa watu wa ngazi ya kata na vijiji mara kwa mara ili kumaliza matatizo hayo katika jamii ya Ruangwa.


from MPEKUZI

Comments