Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) yatoa tahadhari ya mvua nchini

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa tahadhari ya siku tano ya kunyesha mvua kubwa inayoweza kusababisha athari ikiwemo mafuriko.

 Kwa mujibu wa taarifa ya TMA, mvua hizo zinatarajiwa kuanza kunyesha leo Ijumaa Machi 29 hadi Aprili 2, 2019 na kwamba zinaweza kuleta athari kwenye makazi ya watu.

Mvua hiyo inatarajiwa kunyesha katika mikoa ya Rukwa, Mbeya, Iringa, Njombe, Songwe, Ruvuma, Lindi, Mtwara, Morogoro, Dar es Salaam, Tanga, Pwani na Zanzibar.

Pia zinaweza kuleta shida katika usafiri na kusimama kwa muda kwa baadhi ya shughuli za kiuchumi na kijamii. Mamlaka hiyo imesema kuanzia leo hadi Machi 31, 2019 mvua hizo zitanyesha katika mikoa ya Rukwa, Mbeya, Iringa, Njombe, Songwe, Ruvuma, Lindi, Mtwara na Morogoro.

Imeeleza kuwa Aprili Mosi hadi Aprili 2, 2019 mvua hizo zitanyesha katika mikoa ya Rukwa, Mbeya, Iringa, Njombe, Songwe, Ruvuma, Lindi, Mtwara, Morogoro, Dar es Salaam, Tanga, Pwani na Zanzibar.

TMA imeshauri Menejimenti ya Maafa na watoa huduma za dharura pamoja na wadau wengine kuchukua hatua za kuweka mipango stahiki kukabiliana na athari zinazoweza kujitokeza.


from MPEKUZI

Comments