Kikwete aitaka Taasisi ya Sayansi za Bahari wilayani Pangani kuwekeza kwenye utafiti

Rais Mstaafu na Mkuu wa Chuo kikuu cha DSM Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete amesema ili nchi iweze kuendelea na kuwa na uchumi mzuri ni lazima iwe na watafiti wenye uwezo wa kugundua vitu mbalimbali vitakavyo iwezesha Serikali kutatua changamoto za wananchi bila kutegemea nchi nyingine

Dk Kikwete  amesema hayo Machi 29 alipofanya ziara ya kutembelea kituo  cha Utafiti na mafunzo ya ufugaji wa samaki kilichopo Pangani mkoani Tanga kilicho chini  ya Chuo Kikuu cha Dar Es Salaam (UDSM)

“Uwekezaji katika utafiti ndio kichocheo kikubwa ambacho
kinaweza kuwapa mafanikio makubwa muweke msukumo kwenye suala hilo kwani ndilo litakalowapa mafanikio makubwa.

“Nimefurahi sana kwamba taasisi hii ipo kwa ajili ya bahari eneo la viumbe vya majini hakuna taasisi nyingine kubwa kushinda nyie mkibaki kuangalia viumbe vya baharini majini na kusahau na vilivyopo maji baridi kutakuwa na ombwe lakini nafurahi hapa mmeanza kufanya utafiti
wa viumbe wa maji baridi,” Amesema.

Dkt Kikwete amesema taasisi hiyo imeanzishwa kwa ajili ya taaluma kubwa ya viumbe vya bahari huku akiwataka watumie taaluma hiyo kuingiza kwenye viumbe wa maji baridi.

Awali akizungumza wakati akisoma risala Mkurugenzi wa Taasisi ya Sayansi za Bahari Dkt Magreth Kyewalyanga amesema malengo ya kuanzishwa kwa taasisi hiyo ni kutoa mafunzo ya uvunaji endelevu na uzalishaji wa mazao ya samaki bahari.

Amesema katika tafiti za uzalishaji wa mazao ya bahari taasisi hiyo ilianza na kilimo cha mwani na uzalishaji katika miaka ya 80 ikifuatiwa na tafiti za ufugaji wa smaki aina ya mwatiko ikiwemo uzalishaji wa lulu kwenye miaka ya 2000 na hatimaye utafiti wa perege kuanzia mwaka 2009.

Aidha amesema mazao mengine yanayofanyiwa utafiti na majaribio ni pamoja na majongoo bahari ,kaa koko, chaza, Spirulina nk, ambapo tafiti hizo ndio zimechangia sana katika kuwapa ukuaji wa uzalishaji wa viumbe mbalimbali baharini hapa nchini

Naye Mkuu wa wilaya ya Pangani, Zainabu Abdallah
Amesema uwepo wa chuo hicho ni faraja kubwa sana kwao na kitakuwa kichocheo cha maendeleo kwa wakazi wa wilaya hiyo


from MPEKUZI

Comments