Kesi ya Bernad Membe dhidi Cyprian Musiba yapigwa kalenda.

Waziri wa zamani wa Mambo ya Nje, Bernad Membe, leo ametinga Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, kusikiliza kesi yake ya madai ya fidia ya Sh. Bilioni 10 dhidi ya Cyprian Musiba iliyopangwa kusikilizwa mahakamani hapo.
 
Hata hivyo, mahakama hiyo iliyoketi chini ya Jaji Elinaza Luvanda ilishindwa kuanza kusikiliza madai hayo baada ya mlalanikiwa kuwasilisha maombi ya kuomba kuongezewa muda wa kuwasilisha majibu dhidi ya Membe.

Membe aliyekuwa ametinga shati la rangi nyeupe na suruali nyeusi, alifika mahakamani hapo mapema leo saa 3:00asubuh akiwa na wakili wake Jonathan Mndeme.

Upande wa mlalamikiwa uliwasilisha maombi namba 119/2019  ukiomba kuongezewa muda wa kuwasilisha majibu nje ya muda.

Jaji alisema mlalamikaji atawasilisha majibu ya maombi hayo Aprili 12 na mahakama yake itasikiliza Aprili 17, mwaka huu na kwamba kesi ya msingi itasubiri uamuzi wa maombi hayo utakapotolewa.

Musiba anadaiwa kumtuhumu  Membe  kuwa anamhujumu Rais Magufuli, na kwamba mbinu mojawapo ya kukamilisha hujuma hizo ni maandalizi ya  kampeni za kugombea urais 2020.


from MPEKUZI

Comments