FIFA Yamfungia Maisha Mwamuzi Wa Tanzania Kwa Rushwa Na Upangaji Matokeo

Kamati ya Maadili ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Duniani (FIFA) chini ya Mwenyekiti wake Vassilios Skouris imemfungia maisha Mwamuzi wa zamani wa Kimataifa na Katibu wa Chama Cha Waamuzi Tanzania (FRAT) Oden Charles Mbaga kwa kujihusisha na masuala ya rushwa ya upangaji matokeo.
 
Baada ya uchunguzi uliofanyika kuanzia July 11,2018 Mbaga amekutwa na hatia ya kuhusika kwenye upangaji wa matokeo ikiwa ni kinyume na kanuni za Maadili za FIFA.
 
Mbaga amevunja Ibara ya 11 ya Kanuni ya rushwa ya FIFA ya mwaka 2009.
 
Anafungiwa maisha kutojihusisha na shughuli zozote za Mpira wa Miguu katika ngazi ya Kitaifa na Kimataifa kwa mujibu wa Ibara ya 7j ya Kanuni za Maadili za FIFA za mwaka 2018 pamoja na Ibara ya 22 ya Kanuni ya Nidhamu ya FIFA.
 
Aidha Mbaga anatakiwa kulipa faini ya kiasi cha fedha ya Uswis Faranga 200,000 ndani ya siku 30 tokea amepata taarifa hizo na anaweza kulipa kwa fedha ya Swiss au kwa dola za Kimarekani.
 
Vilevile Mbaga anatakiwa kulipa gharama za shauri hilo kiasi cha Faranga za KiSwiss 1,000 ndani ya siku 30 tokea amepata taarifa.
 
Anaweza kukata rufaa kwenye mahakama ya kimichezo ya FIFA CAS,rufaa ambayo inawasilishwa moja kwa moja CAS ndani ya siku 21 tokea maamuzi yalipofanyika na ndani ya siku 10 baada ya kumalizika siku 21.
 
Mbaga ambaye ni Katibu wa Chama cha Waamuzi Tanzania (FRAT) anapoteza sifa ya nafasi hiyo kutokana na adhabu ya kufungiwa maisha kutojihusisha na masuala ya Mpira wa Miguu.


from MPEKUZI

Comments