Waziri Mkuu: Serikali Inahitaji Madaktari na Wauguzi

WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa amesema Serikali inawahitaji madaktari na wauguzi ili waende kutoa huduma katika hospitali, vituo vya afya na zahanati.

Ametoa kauli hiyo leo (Jumatano, Januari 30, 2019) alipozungumza na wanafunzi wa mwaka wa tano wanaosomea udaktari Chuo Kikuu cha Dodoma.

Waziri Mkuu amewataka wanachuo hao wasome kwa bidii ili waweze kufaulu masomo yao na kuapata sifa zitakazowawezesha kuajiriwa au kujiajiri.

Waziri Mkuu  amekutana na wanafunzi hao katika Hospitali ya Benjamin Mkapa, alipokwenda kumjulia hali Mbunge wa Misungwi, Charles Kitwanga.

Akiwa hospitalini hapo, pia Waziri Mkuu alimjulia hali Mkuu wa wilaya ya Bahi, Mwanahamisi Makunda ambaye anamuuguza mtoto wake, Tunu Kikula.

Wengine aliowajulia hali ni pamoja na Mbunge wa Viti Maalum, Sabrina Sungura ambaye amelazwa  hospitalini hapo pamoja na wagonjwa wengine.

Kwa upande wake, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu amewapongeza madaktari hao ambao ni wanafunzi.

Amesema madaktari hao wamekuwa wakitoa msaada mkubwa kwa madaktari bingwa katika kuwahuduma  wagonjwa wanaofika hospitalini hapo.

 (mwisho)

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,


from MPEKUZI

Comments